Translate

Wednesday, November 7, 2012

Polisi Mbeya wafanikiwa kuzima jaribio la kuteka malori ya mafuta yanayosafirisha kwenda nchi jirani kupitia Mbeya,wahusika wapanga mawe barabara ya Mbeya/Tunduma maeneo ya mama john wakiwa na vidumu vitupu vya mafuta,wadai haiwezekani kukosa mafuta ilhali mafuta yanapita machoni pao,wang'ang'ania makufuli ya matenki ya mafuta

Na Thompson Mpanji,Mbeya
 
JESHI la polisi limefanikiwa kuzima jaribio la baadhi ya madereva wa boda boda na daladala kuzuia magari yanayobeba mafuta kusafirisha kwenda nchi za jirani za Zambia baada ya kuamua kuweka kizuizi cha mawe katika barabara ya Mbeya/ Tunduma,katika maeneo ya mama John kwa madai ya kukerwa na adha ya mafuta huku wakiyaona  yakipita kuelekea nchi jirani.
 
Sakata hilo limedumu kwa takribani masaa mawili tangu saa 1 asubuhi hadi saa 3 asubuhi baada ya madereva wa daladala na waendesha boda boda kudaiwa kupandwa na jazba ya kukosa mafuta katika kituo cha Orxy Mama John na hivyo kuamua kupanga mawe barabarani jambo ambalo inadaiwa endapo Polisi wasingejitokeza haraka hali ingekuwa tete kutokana na baadhi yao kuonekana waking'ang'ania makufuli ya malori ya mafuta waliyofanikiwa kuyazuia na kuwateremsha madereva kwa nguvu.
 
"Ninakwambia kulikuwa na hatari kubwa kama wasingetokea wale FFU kwa sababu wengine walitaka kuyapiga kiberiti malori hayo ya mafuta baada ya kuwalazimisha madereva wa magari hayo kufungua nao wakagoma na huku madereva wa malori ya mafuta nao walikuwa wamechukia kwa hiyo tungekuwa tunazungumza kitu kingine,na madereva wengine wa malori walivyopata taarifa kuwa hali siyo shwari waligeuza na kurudi Uyole kuegesha Uyole walivyopata lakini walipotokea maaskari walitawanyika,"alisema mmoja wa wafanyakazi wa kituo hicho cha mafuta ambaye hakutaka kutaja jina lake.
 
Alisema kuwa chanzo cha hasira ya watu hao hawakuamini kama mafuta waliyokuwa wakiyatoa ya petroli kama yamekwisha na kubakiwa na mafuta ya dizeli na hivyo kuanza kupiga kelele na kuhamishia hasira zao barabarani hadi Jeshi la polisi likiongozwa na Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Mbeya Sylivester Ibrahim kuwaaminisha kwa kumuomba mmiliki wa kituo hicho kupima na kuhakikisha kweli hakuna mafuta waliamua kuondoka.
 
Gazeti hili limeshuhudia majira ya saa 4 asubuhi baada ya hali ya utulivu kurejea malori ya mafuta yalionekana yakipita kasi katika maeneo ya mama John tofauti na siku nyingine ambapo taarifa kutoka kituo cha Mafuta cha Uyole yanapoegeshwa magari yanayoelekea Tukuyu kuwa mafuta yapo ila bei ya mafuta ya petroli kwa lita inadaiwa kufikia Sh.3,000.
 
Mmoja wa waendesha boda boda ambaye hakutaka kutaja jina lake alisema wamekerwa sana na kitendo cha kuhangahika na kukosa mafuta kwa takribani siku nne sasa huku magari ya mafuta yakiwa yanapitishwa machoni pao kwenda zambia na kwingineko jambo ambalo alidai bado linawasumbua katika vichwa vyao kuwa serikali inafurahi kero hii wanayoipata walala hoi wa chini huku familia zao zikiendelea kuteseka na njaa kwa kukosa kufanyakazi.
 
Suala hili la ukosefu wa mafuta bado linaonekana ni kitendawili kwa watanzania na kwamba endapo serikali haitalishughulikia na kulimaliza haraka iwezekanavyo kuna hatari ya malori yanayosafirisha mafuta kwenda nchi ya zambia kupitia Mbeya yakafanyiwa hujuma kutokana na kuwepo na tetesi kuwa hawajaridhika kukosa mafuta ilhali wanayaona yanapita mbele ya machjo yao.
 
Hata hivyo Mwandishi wa habari hizi ameshuhudia Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Mbeya,Sylivester,Mkuu wa upelelezi wa Wilaya,Ntatiro,ofisa habari wa Polisi na baadhi ya makachero wakiwa wamesimamia hali ya usalama katika zoezi la utoaji wa mafuta ya Petroli na mafuta ya taa katika kituo cha Total Mafiati huku kukiwa na foleni kubwa ya magari,waendesha boda boda,watu walioshika vidumu vya lita tatu na tano.
 
 
Mwisho.
 

No comments:

Post a Comment