Translate

Friday, May 3, 2013

Watano wanaodhaniwa majambazi wauawa katika majibizano na polisi Mbeya



Na Thompson Mpanji,Mbeya

WATU watano wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wameuawa na Polisi baada ya kutokea  mapambano makali ya kurushiana risasi na askari polisi.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Mbeya,kamishna msaidizi wa polisi,Diwani Athumani amesema tukio hilo limetokea  leo mei,3,2013 majira ya saa 6.00 mchana huko maeneo ya Garijembe,Wilaya ya Mbeya vijijini katika  barabara ya Mbeya-Tukuyu,mkoani Mbeya ambapo kulitokea   mashambulizi ya risasi kati ya askari polisi na watuhumiwa wa ujambazi.

Kamanda Diwani alisema kabla ya kuanza kwa mashambulizi hayo majambazi walishuka katika gari lenye nambari za usajili T.911 BUG aina ya Toyota Spacio rangi ya fedha (silver) mara baada ya kusimamishwa na askari polisi na kuanza kurusha risasi ovyo kwa askari.

Alisema kwa haraka askari walijibu mashambulizi na kuwajeruhi majambazi hao sehemu mbalimbali za miili yao na kwamba silaha walizotumia ni  SMG 848628 ambapo  kwenye magazine zilibakia risasi 16 pamoja na silaha aina ya Mark III namba 94695J na risasi mbili sanjari na koa za shaba zilizokutwa ndani ya gari.

Kamanda Diwani alisema  watuhumiwa  hao watano walikimbizwa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kwa ajili ya matibabu  lakini ilithibitishwa  na daktari  kuwa wamefariki dunia.

Aidha alisema Jeshi  la Polisi lilipokea taarifa  za kiinterejensia kuwa wapo majambazi wanaojipanga kufanya uhalifu kwa wafanyabiashara  katika maeneo  na miji  ya Ushirika na Tukuyu wilayani Rungwe pamoja na Uyole jijijini Mbeya  na kwamba taarifa zilionesha kwamba watakuwa na gari dogo.

Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya ametoa wito kwa yeyote mwenye taarifa  zinazohusu uhalifu na wahalifu azitoe katika mamlaka husika kwa wakati ili zifanyiwe kazi kwa haraka.

Hata hivyo Kamnada Diwani ameendelea kutoa onyo kwa watu wanaoendelea kutegemea kufanya uhalifu kama njia ya kujipatia kipato kuachana na shughuli hiyo kwani hawataweza kufanikiwa.

Mwisho.