Translate

Monday, March 25, 2013

Kardinali Pengo aadhimisha Ibada ya Jumapili ya Matawi Jimboni Zanzibar na kutoa salam za Papa Francisko

Kardinali Pengo aadhimisha Ibada ya Jumapili ya Matawi Jimboni Zanzibar na kutoa salam za Papa Francisko



Baba Mtakatifu Francisiko hivi karibuni, alikutana na kuzungumza na wawakilishi wa dini na madhehebu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, akikazia kwa namna ya pekee majadiliano katika upendo na ukweli na kwamba, Kanisa Katoliki linapania kujenga na kuimarisha majadiliano ya kidini na kiekumene na waamini wa dini na madhehebu mbali mbali ya Kikristo. Kanisa linapenda kujielekeza pia katika majadiliano na wale wasiokuwa na dini maalum, ambao daima wana kiu ya kutaka kumfahamu Mungu kutoka katika undani wao.

Baba Mtakatifu Francisiko anakumbusha kwamba, Wakristo na Waislam wana mwamini Mungu mmoja, aliye hai ambaye pia ni mwingi wa huruma na upendo; waamini wa dini hizi wanamwendea wote kwa njia ya sala, changamoto ya kujenga na kudumisha ushirikiano wa dhati baina ya Wakristo na Waislam kwa ajili ya mafao na ustawi wa binadamu wote. Kuna haja ya kuendeleza urafiki na heshima kila mtu; daima wakisimama pamoja kulinda na kutetea kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amedhaminishwa na Mwenyezi Mungu.

Wakristo na Waislam anasema Baba Mtakatifu Francisko, wanaweza kujibidisha zaidi kwa ajili ya kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; kwa kujikita katika upatanisho na ujenzi wa amani ya kudumu; lakini jambo la msingi ni kushirikiana kwa pamoja ili kuzima kiu ya uwepo wa Mungu inayooneshwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Hii ndiyo changamoto ambayo Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam aliyopeleka Jimboni Zanzibar, katika Maadhimisho ya Jumapili ya Matawi, ambayo kwa mwaka huu, ilikuwa na nafasi ya pekee katika moyo wa Baba Mtakatifu Francisko aliyemtuma Kardinali Pengo kumwasilishia salam na matashi mema kwa Wakristo wa Zanzibar ambao wamepitia kipindi kigumu katika miaka ya hivi karibuni.

Kardinali Pengo katika mahubiri yake, kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Yosefu, Jimbo Katoliki la Zanzibar, amekazia kwa mara nyingine tena umoja, upendo na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa dini mbali mbali nchini Tanzania na kamwe tofauti zao za kiimani zisiwe ni chanzo cha vurugu na chokochoko za kiimani. Hakuna mtu anayeweza kuhalalisha mauaji ya binadamu mwingine kwa madai ya kwamba, anatetea imani kwa Mungu aliye asili na uhai.

Kardinali Pengo ametumia fursa hii pia kuwataka Wazanzibar kutunza mazingira kwa ajili ya mafao ya sasa na yale ya kizazi kijacho. Kuna wakati Zanzibar ilikuwa inatoa maji safi ya kunywa, lakini sasa maji mengi ni ya chumvi. Utunzaji wa mazingira ni jambo linalopaswa kupewa msukumo wa pekee na Jamii na wala hawapaswi kulipuuzia.

Wednesday, March 20, 2013

Maskini hata katika umaskini wao wanaweza kuchangia kwa hali na mali kulistawisha Kanisa



Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Afrika na Madagascar, SECAM, katika mahojiano na Radio Vatican anasema kwamba, kwake binafsi anaona kwamba, kuchaguliwa kwa Baba Mtakatifu Francisko kuliongoza Kanisa Katoliki ni paji la Roho Mtakatifu kwa Kanisa la Ulimwengu mamboleo na kwa namna ya pekee kwa Kanisa Barani Afrika. RealAudioMP3

Katika ulimwengu mamboleo watu wamefikia hatua ya kudhani kwamba, kwa nguvu ya fedha, mali na uchumi wanaweza kufanya jambo lolote hapa duniani. Baba Mtakatifu Francisko ni baraka kwa Kanisa, hali inayojionesha hata katika uchaguzi wa jina lenyewe. Ni Mtakatifu aliyezaliwa na kulelewa katika familia iliyobahatika kuwa na utajiri mkubwa.

Baada ya kuongoka akaacha yote na kujitosa pamoja na wenzake kumjengea Kristo Kanisa. Mwanzoni alidhani ni Kanisa la mawe, lakini pole pole alitambua kwamba, Kanisa alilokuwa anapewa changamoto ya kulijenga ni Fumbo la Mwili wa Kristo, kwa njia ya ushuhuda wa maisha yanayojikita katika ufukara kwa kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu.

Kardinali Pengo anakumbusha kwamba, Mwenyezi Mungu ana njia zake na kamwe hawezi kufungwa na fikara na mawazo ya binadamu. Uamuzi wa Francisko ulikuwa ni mzito, kiasi kwamba, baba yake mzazi aliamua kufukuza kutoka nyumbani kwake.

Francisko akapewa changamoto ya kulijenga Kanisa la Kristo lililokuwa limeanza kumezwa na malimwengu,kwa kutaka mambo ya ufahari na mali, katika ulimwengu wa wakati ule! Watu walipima mafanikio kwa wingi wa mali na madaraka aliyokuwa nayo mtu, wakasahau kwamba, madaraka ni kwa ajili ya kuwahudumia wanyonge na maskini na kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye chimbuko la mafanikio ya binadamu.

Kardinali Polycarp Pengo anasema, Baba Mtakatifu Francisko alikwisha kuona na kuonja hadha ya umaskini na mahangaiko ya watu wa Argentina. Akatambua kwamba, hawa ndio tegemeo la Kanisa. Akajitosa bila ya kujibakiza hata kidogo, akasimama kidete kulinda na kuwatetea maskini, ambayo kwa uhuru kamili amethubutu wawepo kwenye Ibada ya Misa Takatifu alipokuwa anaanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu Francisko hata baada ya kuchaguliwa kwake, maneno yake ya kwanza kwanza yanayonesha changamoto kwa Kanisa katika kuwahudumia maskini na kwamba, uongozi hauna budi kuwa ni huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ni changamoto ambayo imeendelea kusikika hata katika Mahubiri yake kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Siku ya Jumanne, tarehe 19 Machi 2013.

Kardinali Polycarp Pengo anasema, Waamini Barani Afrika hata katika umaskini wao, wanaweza kuchangia kwa hali na mali katika ustawi na maendeleo ya Kanisa Barani Afrika. Hakuna sababu ya kukata tamaa na kwamba, umaskini au ufukara wa Kiinjili si jambo linaloweza kuwa ni kikwazo cha kuchangia maendeleo ya Kanisa Barani Afrika.

Hii ni changamoto kwa waamini Barani Afrika kushikamana na kujifunga kibwebwe kutumia karama na vipaji walivyokirimiwa na Roho Mtakatifu kwa ajili ya maendeleo ya Kanisa na Jamii kwa ujumla wake. Wawe tayari kumsikiliza Mwenyezi Mungu anayezungumza nao kutoka katika undani wa dhamiri zao nyofu na kamwe kisiwepo kisingizio tena!

Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM anahitimisha mahojiano haya maalum na Radio Vatican kwa kutolea ushuhuda jinsi ambavyo hata Makardinali walivyopigwa na butwaa walipomwona Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kushirikiana nao kwa sala, chakula na maongezi kama ndugu bila ya kujitenga, changamoto kubwa kwa sasa ni kumsikiliza, kuona na kutenda kadiri ya maongozi yake!

Tuesday, March 19, 2013

Shutuma dhidi ya Kardinali Bergoglio hazina msingi wowote!




Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, kampeni za kutaka kumchafua Kardinali Jorge Mario Bergoglio, ambaye kwa sasa ni Baba Mtakatifu Francis, zimechapishwa na gazeti moja ambalo linajipambanua kwa kampeni chafu za kutaka kuwapaka watu matope. Ni gazeti ambalo limekuwa likiendesha kampeni dhidi ya Makleri, kiasi kwamba, si jambo la kushangaza kusikia gazeti hili limeibuka kwa mara nyingine tena kutaka kumchafua Kardinali Bergoglio.

Shutuma zinazotolewa na gazeti hili zinapata chimbuko lake, wakati Bergoglio alipokuwa nchini Argentina kama Mkuu wa Shirika la Wayesuit, pale ambapo Mapadre wawili walipotekwa nyara na kwamba, hakuweza kutoa kinga dhidi ya Mapadre hao wasitekwe nyara.

Padre Lombardi anafafanua kwamba, shutuma hizi hazina msingi wowote. Vyombo vya sheria nchini Argentina wakati fulani vilimhoji kuhusu shutuma hizi, lakini hakuna hata siku moja vilipomkuta na hatia wala shitaka la kujibu. Mhusika mwenyewe alikana shutuma hizi na kuhifadhiwa.

Padre Lombardi anabainisha kwamba, kuna vielelezo na ushahidi mkubwa kutoka kwa watu mbali mbali wanaonesha kwamba, Bergoglio aliwalinda na kuwapatia hifadhi wakati wa madhulumu nchini Argentina, pale nchi ilipokuwa inatawaliwa kwa mtutu wa bunduki.

Mchango wa Bergoglio unafahamika sana, pale alipoteuliwa kuwa Askofu, alipoanzisha mchakato wa kuomba msamaha kwa ajili ya Kanisa la Argentina kwamba, wakati wa madhulumu, Kanisa Katoliki halikujishughulisha sana kuwalinda na kuwatetea wanyonge na wote waliokuwa wanadhulumiwa na utawala wa Kidikteta.

Shutuma hizi zinafumbatwa katika upembuzi yakinifu wa masuala ya kihistoria na kijamii wakati wa utawala wa kidikteta, zilizofanywa na makundi dhidi ya Makleri, kama njia ya kulishambulia Kanisa. Shutuma zote hizi hazina msingi na lazima zipingwe kwa kauli moja. Ndivyo Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anavyohitimisha maneno yake dhidi ya shutuma zinazolenga kumpaka matope Kardinali Bergoglio.

Papa Francisko amwagiza Kardinali Pengo kuwaimarisha Zanzibar,na habari nyingine za papa ukurasa huu



Serikali ya Tanzania yatuma salam za pongezi kwa Papa Francis
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://media01.radiovaticana.va/imm/1_0_673895.JPGRais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania, Ijumaa 15 Machi, 2013 amemtumia salamu za Pongezi Baba Mtakatifu Francis kwa kuchaguliwa kwake kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro na kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki.

“Kuchaguliwa kwako ni ushuhuda tosha wa imani na heshima kubwa ambayo Kanisa Katoliki inayo kwako, historia yako na upendo wako wa kujali na kuwapenda wanyonge, unyenyekevu ni sababu tosha ya kuwapa Wakatoliki, wasio Wakatoliki na wasio Wakristo pia kusherehekea uteuzi wako” Rais Kikwete amesema kwenye barua yake ya Pongezi kwa Papa Francis .

Vatican na Tanzania imekua na uhusiano wa muda mrefu na hivyo Rais Kikwete amemhakikishia Papa Francis kuwa uhusiano huo utadumu na anatarajia utaimarika zaidi chini ya uongozi mpya wa Papa Francis.


Papa Francisko amtuma Kardinali Pengo kuwaimarisha ndugu zake katika imani Visiwani Zanzibar
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://media01.radiovaticana.va/imm/1_0_674718.JPGKardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar ambaye pia ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Tanzania, katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema, hivi karibuni alipokutana na Baba Mtakatifu Francisko, alimtuma kwenda Zanzibar ili kuwaimarisha ndugu zake katika imani. RealAudioMP3

Kutokana na agizo hili, Kardinali Polycarp Pengo, anatarajiwa katika maadhimisho ya Jumapili ya Matawi, kushiriki na waamini wa Jimbo Katoliki Zanzibar kwa Ibada inayoliingiza Kanisa katika Maadhimisho ya Fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Kristo.

Kardinali Polycarp Pengo anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumwombea Baba Mtakatifu Francisko, ili Mwenyezi Mungu aweze kumlinda na kumwiimarisha katika utekelezaji wa malengo yake ya kitume. Papa Francisko akiishaimarika katika imani, matumaini na mapendo, aweze pia kuwaimarisha ndugu zake katika Kristo, hasa wale wanaoishi katika wasi wasi na hofu ya madhulumu ya kidini. Wasikie na kuonja uwepo na sala za Baba Mtakatifu Francisko katika hija ya maisha yao hapa duniani, kamwe wasidhani kwamba, wamesahaulika!

Mamia ya maelfu watarajiwa kuhudhuria Ibada ya Papa Francis kuzindua utawala wake wa kitume, Jumanne: Hakuna kiingilio wala tiketi.

http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://media01.radiovaticana.va/imm/1_0_674408.JPGSiku ya Jumanne Machi 19, 2013, ambamo Mama Kanisa ana adhimisha Siku Kuu ya Mtakatifu Yosefu Mchumba wa Bikira Maria, na Msimamizi wa Kanisa la Ulimwengu, majira ya asubuhi ya saa tatu na nusu za asubuhi, (saa za Roma), Papa Francis, ataongoza Ibada ya Misa Takatifu , kama alama rasmi ya kuzindua utume na utawale wake wa Kipapa katika kiti cha Mtume Petro.

Mamia ya maelfu ya mahujaji na wageni wanatarajiwa kuujaza uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, kwa ajili hiyo. waamini wote mnatagaziwa kwamba Ibada hii ni wazi kwa wote na hakuna haja ya kuwa na tiketi kama kiingilio.

Ibada hii, itatangazwa moja kwa moja na vituo vingi vya redio, televisheni na njia nyingine za mpya za mawasiliano, kama itakavyo sikika moja kwa moja pia katika tovuti za Radio Vatican.
Katika Ibada hii, viongozi na Wajumbe rasmi wa viongozi wa kidini na kisiasa watakuwepo.Vivyo hivyo Makardinali wote, Maaskofu Wakuu na Maaskofu kadhaa kutoka pande mbalimbali za dunia, wameteuliwa kuja kuwakilisha makanisa mahalia na kuionyesdha sura ya kanisa la Kanisa la Ulimwengu.
Na kwamba Patriaki wa Kiekuemeni wa Constantinople, Bartholomayo I, ambaye ni huchukuliwa katika nafasi sawa na Papa katika Usharika wa Kanisa la Kiotodosi la Mashariki,pia anatarajia kuandika historia ya mpya ya kushiriki ibada hii kwa mara ya kwanza. Na Jumuiya ya Kianglikani duniani , inawakilishwa na Askofu Mkuu wa York Uingereza , Dr. John Sentamu, anayemwakilishi kiongozi mkuu wa Jumuiya hiyo, Askofu Mkuu wa Canterbury, kama itakavyo kuwa pia uwepo wawakilishi wa imani na tamaduni zingine kubwa duniani.
Kwa dunia ya Kisiasa , kati ya wanaotarajiwa kuwepo ni pamoja na Rais wa Argentina Cristina Kirchner, pia Rais Dilma Rousseff Rais wa Brazil, na Rais Enrique Peña Nieto, Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe, na Mwana Mfalme wa Uingereza anayemwakilisha Malkia Elizabeth 11 . Rais Obama wa Marekani anawakilishwa na Makamu wake Joe Biden, na Gavana Mkuu wa Canada, Daudi Johnston.
Wengine watakao kuwepo katika uzinduzi huu, ni pamoja na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel, Waziri Mkuu wa Ufaransa Jean-Marc Ayrault na Waziri Mkuu-Waziri Mariano Rajoy wa Hispania. Na Rais wa Baraza la Ulaya, Herman Van Rompuy, na Rais wa Tume ya Ulaya, José Manuel Barroso, wote wameonyesha nia za kuhudhuria, kwa kutaja wachache.
Papa Francis , anazindua kazi zake kama Askofu wa Roma na Mkuu wa Kanisa Katoliki la ulimwengu baada ya kuchaguliwa na Makardinali siku ya Jumatano illiyopita katika kura ya siri iliyopigwa kikao cha Conlave, nyakati za jioni. Na Ibada hii ya Jumanne , ni alama ya mwanzo kabisa ya utawala wake kama khalifa wa Mtume Petro.

Wasifu wa Baba Mtakatifu Francis!

http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
Baba Mtakatifu Francis ni Myesuiti wa kwanza kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni Papa wa kwanza katika historia ya Kanisa kutoka nje ya Bara la Ulaya na Papa wa kwanza katika historia ya Kanisa kutoka katika nchi za Amerika ya Kusini, nchi ambazo kwa sasa zina idadi kubwa ya waamini wa Kanisa Katoliki. Kwa mara ya kwanza Jina la Mtakatifu Francis linatumiwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Lakini ikumbukwe kwamba, kuna watakatifu wanne wenye majina ya Francis. Hawa ni akina Mtakatifu Francis wa Assisi, Msimamizi wa Italia; Mtakatifu Francis wa Sale, Mwalimu wa Kanisa na Msimamizi wa Waandishi wa Habari; Mtakatifu Francis Xsaveri, Myesuit na Msimamizi wa Wamissionari pamoja na Mtakatifu Francis wa Paulo, Mkaa pweke na mwanzilishi wa Shirika la Ndugu wadogo wa Calabria.

Kardinali Jorge Mario Bergoglio, SJ, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires, Argentina, alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 mjini Buenos Aires. Yeye ni mtoto wa Mzee Mario na Mama Regina Sivori, waliobahatika kupata watoto watano. Katika ujana wake, alisoma na kufuzu kama mtaalam wa kemia, baadaye akaacha kazi hii na kujiunga Seminarini huko Villa Devoto.

Tarehe 11 Machi 1958 alijiunga na malezi ya Kinovisi katika Shirika la Wayesuit akaendelea pia na masomo dunia nchini Cile na kunako mwaka 1963 alirejea tena Buenos Aires na kujipatia shahada ya uzamili kutoka katika Kitivo cha Falsafa, Chuo Kikuu cha San Josè huko San Miguel.

Kati ya mwaka 1964 na mwaka 1965 alikuwa ni Jaalim wa Fasihi Andishi na Saikolojia katika Chuo cha Bikira Maria wa Santa Fe. Kunako mwaka 1966 akafundisha masomo haya kwenye Chuo Kikuu cha Salvatore cha Buenos Aires. Kuanzia mwaka 1967 hadi mwaka 1970, alijiendeleza kwa masomo ya Taalimungu katika Chuo Kikuu cha San Josè kilichoko San Miguel na kujipatia shahada ya uzamili.

Tarehe 13 Desemba 1969 akapewa daraja takatifu la Upadre. Kati ya mwaka 1970 hadi mwaka 1971 alikamilisha hatua ya tatu ya majiundo yake kama Myesuit huko Hispania na tarehe 22 Aprili 1973 akaweka nadhiri za daima. Kati ya mwaka 1972 hadi mwaka 1973 alikuwa ni mlezi wa Wanovisi, Jaalim, Mshauri na Gombera wa Chuo cha Massimo. Tarehe 31 Julai 1973 akateuliwa kuwa Mkuu wa Jimbo la Argentina kwa upande wa Shirika, utume ambao aliutekeleza kwa muda wa miaka 6. Kati ya Mwaka 1980 hadi mwaka 1986, alikuwa ni Gombera wa Chuo cha Massimo na Paroko wa Parokia ya Patriaki San Josè, Jimboni San Miguel.

Kunako mwaka 1986 alikwenda nchini Ujerumani kumalizia masomo yake katika Shahada ya Uzamivu na wakuu wake wa Shirika wakampatia jukumu la kuwa mkuu wa malezi ya kiroho na muungamishi katika Chuo cha Salvatore.

Tarehe 20 Mei 1992 Papa Yohane Paulo II akamteuwa kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires, akawekwa wakfu kama Askofu tarehe 27 Juni 1992. Tarehe 3 Juni 1997 akateuliwa kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires na tarehe 28 Februari 1998 akasimikwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires baada ya kifo cha Kardinali Antonio Quarracino na hivyo kuwa pia ni Mkuu wa Kanisa Katoliki Argentina.

Mwenyeheri Yohane Paulo II akamteuwa na kumsimika kuwa Kardinali kunako tarehe 21 februari 2001. Ameshiriki katika Sinodi ya Maaskofu iliyofanyika kunako mwaka 2001. Akashiriki pia kwenye mkutano wa Makardinali wakati wa uchaguzi wa Papa kati ya tarehe 18 na 19 Aprili 2005. Alikuwa ni mjumbe wa Halmashauri ya Sinodi ya kumi na moja ya Maaskofu kuanzia tarehe 2 hadi 23 Oktoba 2005.

Mjini Vatican alikuwa ni mjumbe wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri, Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Tume ya Kipapa ya Amerika ya Kusini, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri na Mjumbe wa Sekretarieti ya Sinodi.

Nchini Argentina alikuwa ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Argentina.
Rais wa Tume ya Baraza la Maaskofu kwa ajili ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Argentina. Alikuwa ni mratibu mkuu wa Mahakama ya Kanisa; Mratibu wa Mahakama ya Jimbo kuu la Buonos Aires. Tangu mwaka 2005 hadi 2011 alikuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina.
Ni mwandishi wa Vitabu vifuatavyo:
1982: Meditaciones para religiosos
1986: Reflexiones sobre la vida apostólica
1992: Reflexiones de esperanza
1998: Diálogos entre Juan Pablo II y Fidel Castro
2003: Educar: exigencia y pasión
2004: Ponerse la patria al hombro
2005: La nación por construir
2006: Corrupción y pecado
2006: Sobre la acusación de sí mismo
2007: El verdadero poder es el servicio
Baba Mtakatifu Francis ni kiongozi anayetaka kutoa huduma kwa Kanisa la Kristo!
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://media01.radiovaticana.va/imm/1_0_673228.JPGPadre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Kanisa limempokea kwa mikono miwili, Baba Mtakatifu Francis anayetoka Amerika ya Kusini ambako kwa sasa Kanisa lina waamini wengi wenye fursa na changamoto katika maisha na utume wa Kanisa.

Uchaguzi wa Jina la Francis una maana kubwa katika maisha na utume wa Papa Francis, jina amblo kwa mara ya kwanza linatumika katika historia ya Kanisa kwa ajili ya Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni jina linalobainisha unyofu na ushuhuda wa Kiinjili, mambo ambayo yamejionesha kwa Baba Mtakatifu alipotokeza hadharani kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican hapo Jumatano tarehe 13 Machi 2013.

Ameonesha unyenyekevu wa hali ya juu kwa kuomba sala na baraka kutoka kwa waamini na watu wenye mapenzi mema, kabla hata ya Yeye mwenyewe kuwapatia baraka yake ya kitume! Ni mtu wa sala, kama ilivyojionesha pia wakati akizungumza na waamini wa Jimbo kuu la Roma. Inapendeza kuona Familia ya Mungu inasali kwa pamoja.

Baba Mtakatifu Francis ni Myesuit na Wayesuit wanajipambanua na Watawa wa Mashirika mengine kwa njia ya huduma kwa Kanisa, kwa kuhakikisha kwamba, wanatumia karama na mapaji waliyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa. Uongozi ni huduma na wala si uchu wa madaraka!

Huu ndio mwelekeo unaoneshwa na Kanisa kwa wakati huu kwamba, watu wanaalikwa kuhudumia na kwamba Baba Mtakatifu Francis ni mtu anayeonesha kwamba, kweli anataka kulihudumia Kanisa, kwani uchaguzi wake umekuja wakati ambapo Papa Benedikto wa kumi na sita, alipoamua kung'atuka madarakani, kielelezo cha hali ya juu kabisa cha huduma kwa Mungu na jirani, kwa kutambua uwezo na umri wake.

Baba Mtakatifu Francis amezungumza tayari kwa njia ya simu na Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita na kwamba, anaendelea kumwombea katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.


Ataitwa "Baba Mtakatifu mstaafu"
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
http://sw.radiovaticana.va/global_images/x.gif
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita baada ya kung'atuka rasmi madarakani hapo tarehe 28 Februari 2013, saa 2:00 Usiku ataanza kuitwa "Baba Mtakatifu Mstaafu". Ufafanuzi huu umetolewa na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican baada ya wanasheria wa Kanisa kukaa na kulitafakari tukio hili la kihistoria katika maisha na utume wa Kanisa.

Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro tayari umesheheni waamini, mahujaji na watu wenye mapenzi mema kutoka sehemu mbali mbali za dunia waliofika kutoka heshima zao za mwisho kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ratiba inaonesha kwamba, Alhamisi, tarehe 28 Februari 2013, Majira ya asubuhi, Baba Mtakatifu anatarajiwa kukutana na Makardinali ambao wamekwisha wasili hapa mjini Roma kwa ajili ya mazungumzo ya faragha. Jioni ataagwa rasmi na Vikosi vya Ulinzi na Usalama mjini Vatican. Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican ataongoza ujumbe wa viongozi waandamizi kutoka Vatican watakaomuaga Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kabla ya kuondoka rasmi mjini Vatican kuelekea kwenye Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo, nje kidogo ya mji wa Roma.

Baba Mtakatifu anatarajiwa kufika jioni mjini Castel Gandolfo, na huko atapokelewa na Kardinali Giuseppe Bertello, Gavana wa Mji wa Vatican pamoja na Askofu mkuu Giuseppe Sciacca, katibu mkuu wa Gavana wa Vatican, Askofu Marcello Semeraro wa Jimbo la Albano pamoja na viongozi wa Serikali. Atakapo wasili Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo, Baba Mtakatifu atatokeza dirishani kusalimiana na wananchi pamoja na wageni watakaokuwa wamefika mjini Albano. Saa 2:00 Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, atakuwa anang'atuka rasmi kutoka madarakani na tangu wakati huo Kiti cha Ukulu wa Mtakatifu Petro kitakuwa wazi.

Walinzi wa kutoka kutoka Uswiss ambao wamepewa dhamana maalum ya kumlinda Khalifa wa Mtakatifu Petro, kadiri ya Mapokeo ya Kanisa, watakuwa wamemaliza utume wao na kurudi makao makuu ya Vikosi hivi mjini Vatican. Vikosi vya ulinzi na usalama kutoka Vatican vitaendelea kushughulikia masuala ya ulinzi na usalama wa Papa mstaafu. Tangu wakati huo, Baba Mtakatifu hatavaa tena ile "Pete ya Mvuvi" inayoonesha ukulu wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro wala hata vaa tena vile viatu vyekundu alama ya ushuhuda wa imani hata ikibidi kumwaga damu!

Padre Lombardi anasema kwamba, mwanzo mwa Mwezi Machi, Dekano wa Makardinali, atatuma barua ya mwaliko kwa Makardinali wote ili kushiriki katika Mkutano wa Dekania ya Makardinali utakaokuwa na dhamana ya kuanza mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya. Mikutano ya Makardinali inatarajiwa pia kuanza Juma lijalo. Mikutano hii itafanyika kwenye Ukumbi Mpya wa Sinodi.

Kutokana na sababu za kiufundi, Padre Lombardi anasema, Makardinali watahamia kwenye Hosteli ya Mtakatifu Martha iliyoko mjini Vatican, siku moja kabla ya uchaguzi wa Papa Mpya. Utaratibu wote utapangwa wakati wa mkutano wa Makardinali. Kikanisa cha Sistina ambacho kina utajiri mkubwa wa Sanaa kitafungwa rasmi kuanzia tarehe 28 Februari 2013 ili kutoa nafasi kwa ajili ya maandalizi ya mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya.


Wednesday, March 13, 2013

Amina Nganile akiwa na mwanawe muda mfupi baada ya kujifunguwa katika Hospitali ya ifisi ambapo alidaiwa kuuzwa mtoto huyo kwa wazungu

Bw.Mervin Kauffman akiwa na mke wake Anna aliyemshika mtoto wa Amina Nganile aliyedaiwa kuuzwa,pamoja na watoto wengine wanaolelewa na familia hiyo Joseph na Esther na watoto wao katika picha ya pamoja

Awamu ya tatu, bado moshi ni mweusi! Vuteni subira!

   Maskani > Kanisa >  2013-03-13 11:02:59
A+ A- Chapisha ukurasa huu Tuma kwa e-mail






Makardinali 115 wenye dhamana ya kupiga na kupigiwa kura, Jumatano, tarehe 13 Machi 2013, baada ya maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, waliingia kwenye Kikanisa cha Sistina kwa ajili ya kusali masifu ya asubuhi na baadaye wakaendelea na mchakato wa kupiga kura.

Leo Makardinali wanatarajia kupiga kura mbili asubuhi na mbili jioni. Wakati wote huu, macho na masikio ya waamini na watu wenye mapenzi mema yanaendelea kuelekezwa kwenye Paa la Kikanisa cha Sistina, kitakachotoa alama ya moshi mweupe alama ya kwamba Kanisa limempata Papa Mpya; moshi mweusi, alama kwamba, mchakato bado unaendelea!

Waamini wanakumbushwa kwamba, uchaguzi wa Papa ni tofauti kabisa na uchaguzi unaofanywa katika medani za kisiasa au katika uchaguzi wa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Kimataifa. Hapa Makardinali wamekusanyika kwa ajili ya kumchagua Kiongozi wa Kanisa, atakayepewa dhamana ya kuongoza Jumuiya ya Waamini. Kumbe, yule atakeyechaguliwa kwanza kabisa hana budi kuwa na sifa njema za maisha ya kiroho: mchamungu, anayejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili kutangaza kweli za Kiinjili, mtu anayeaminika na kukubalika na Kanisa na Jamii ya watu wanaomzunguka.

Conclave ni kipindi maalum cha imani, matumaini, mapendo na mshikamano miongoni mwa Makardinali na Kanisa kwa ujumla, ndiyo maana Waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kuwasindikiza Makardinali katika sala. Conclave ni tukio la Liturujia ya Kanisa inayoadhimishwa kwenye Kikanisa cha Sistina, chenye utajiri mkubwa wa sanaa, kinachotoa fursa kwa Makardinali: kusali na kutafakari maajabu na ukuu wa Mungu, wakitambua dhamana waliyokabidhiwa na Kanisa ya kuchagua Kiongozi mkuu.

Hapa hakuna mgawanyiko kama baadhi ya wanahabari wanavyotaka kuwaaminisha wasomaji, watazamaji na wasikilizaji wao! Katika mikutano elekezi, Makardinali wamezungumza katika ukweli na uwazi; mwanga wa Kanisa na Vivuli vinavyoliandama Kanisa; yote haya yamefanyika katika matumaini, utulivu wa ndani na uhuru kamili. Makardinali wakikamilisha mchakato wa uchaguzi, ulimwengu utafahaamishwa mara moja!

Itakumbukwa kwamba, kila siku, Makardinali kadiri ya Misale ya Conclave, wanaweza kuchagua nia ya misa moja kwa ajili ya mahitaji ya Kanisa: kwanza kabisa kwa kufuata liturujia ya siku; kumwomba Roho Mtakatifu; kusali kwa ajili ya Kanisa zima; kumwomba Bikira Maria au kusali kwa ajili ya maombezi ya Watakatifu Petro na Paulo.

Macho ya waamini yameelekezwa kwenye Kikanisa cha Sistina



Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumanne tarehe 12 Machi 2013 ulifurika umati wa waamini, mahujaji na watalii kushuhudia Makardinali wakila kiapo na hatimaye kuanza mkutano wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Licha ya hali mbaya ya hewa, lakini waamini wakiwa na miamvuli yao, waliendelea kusubiri kwa hamu kufahamu walau matokeo ya kwanza ya uchaguzi wa Papa Mpya.

Ilikuwa ni saa 1: 41 Usiku, kwa saa za Ulaya, sauti kubwa ilipotanda Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kwa kuona moshi mweusi, dalili kwamba, bado Makardinali walikuwa hawajafulu kumchagua Papa Mpya.

Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura, Jumatano wameendelea na ratiba yao kama kawaida kwa kupiga kura mara nne, yaani kura mbili asubuhi na kura nyingine mbili nyakati za jioni. Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano yamewawezesha mamillioni ya waamini na watu wenye mapenzi mema kufuatilia mchakato wa uchaguzi wa Baba Mtakatifu moja kwa moja kutoka katika Kikanisa cha Sistina, tangu pale Makardinali walipoanza maandamano kutoka kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Paulo, walipoingia kwenye Kikanisa cha Sistina, wakaanza kula kiapo hadi pale Monsinyo Guido Marini alipofunga lango la Kikanisa cha Sistina, ili kutoa nafasi kwa Makardinali kuanza rasmi mchakato wa kupiga kura.

Kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kuliwekwe Televisheni kubwa nne, zilizowawezesha waamini kufuatilia hatua kwa hatua mchakato mzima wa Conclave, hadi pale moshi mweusi ulipotoka. Ilikuwa ni nafasi kwa waamini pia kuwatambua Makardinali kwa sura kwani wengi wao wamesikika kwa majina, lakini ni wachache waliokuwa wanafahamika zaidi. Katika matukio kama haya havikosekani vituko! Lakini, macho na imani ya watu wengi ni kufahamu nani kati ya Makardinali amechaguliwa kuliongoza Kanisa.

Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo cha Upendo, Umoja na Mshikamano wa Kanisa




Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali, Jumanne tarehe 12 Machi 2013 ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kwa ajili ya kuombea uchaguzi wa Papa Mpya, kielelezo makini cha upendo, umoja na utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Waamini wamekusanyika kwa ajili kumwabudu, kumshukuru na kumwomba Mwenyezi Mungu, ambaye kwa njia ya upendo wake ameendelea kulisimamia, kuliongoza na kuliimarisha Kanisa kwa njia ya Roho Mtakatifu.

Kardinali Sodano amemshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa uongozi wake makini kwa Kanisa na kwamba, sasa Makardinali wanaanza uchaguzi wa Papa wa 265. Kanisa linamwomba Mwenyezi Mungu aweze kulikirimia Kiongozi mwema kwa ajili ya Kanisa lake. Huyu ndiye anayetumwa kuwahubiria wanyenyekevu Habari Njema ya Wokovu; kuwaganga wale waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari ya kufunguliwa kwao, kutangaza Mwaka wa Bwana uliokubalika.

Kardinali Sodano anasema kwamba, utabiri huu umepata utimilifu wake kwa njia ya Yesu Kristo, aliyekuja kuwaonjesha watu upendo wa Mungu, kwa wote wanaoteseka, wanaokabiliana na ukosefu wa haki msingi za binadamu, umaskini pamoja na kumong'onyoka kwa maadili na utu wema. Wote hawa wanahitaji kuona huruma ya Mungu, utume ambao unatekelezwa na viongozi wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee na Khalifa wa Mtakatifu Petro, ambaye baada ya kuonesha upendo mkuu kwa Kristo, alikabidhiwa dhamana ya kuwachunga Kondoo wake. Hii ni huduma ya upendo inayotekelezwa mintarafu mwanga wa Injili na nguvu ya neema.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2013 alibainisha kwamba, kilele cha matendo ya huruma kinajionesha kwa njia ya Uinjilishaji; yaani huduma ya Neno la Mungu pamoja na adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, linalowahusisha na kuwachangamotisha Watu wa Mungu kujenga na kuimarisha uhusiano na Muumba wao.

Uinjilishaji ni kielelezo cha hali ya juu kabisa cha huduma kwa binadamu na kwamba, Yesu Kristo ni nguzo msingi katika mchakato wa maendeleo endelevu, kama alivyobainisha Papa Paulo wa sita, katika Waraka wake juu ya Maendeleo ya Watu.

Kardinali Angelo Sodano anasema kwamba, Neno la Mungu limefafanua kwa dhati kabisa juu ya Fumbo Kristo na Kanisa lake; umuhimu wa kujenga na kuimarisha umoja wa Kanisa, kila mtu kadiri ya karama aliyopokea, akitekeleza wajibu wake katika fadhila ya upendo na amani. Umoja huu unasimikwa katika utofauti wa karama na majukumu, lakini kwa pamoja unapania kujenga na kuimarisha Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Huu ndio umoja unaojengwa na kuimarishwa na Roho Mtakatifu na kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo wazi cha umoja wa Kanisa, changamoto kwa kila mwamini kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa umoja wa Kanisa.

Kardinali Sodano anasema amri kuu ambayo Kristo aliwaachia mitume wake, ile siku iliyotangulia kuteswa kwake ni upendo. Huu ndio mhimiri mkuu wa Viongozi wa Kanisa, wanaosukumwa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ndugu zao katika Kristo. Huu ni wajibu mkubwa kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro anayepaswa kuonesha upendo huu kwa Kanisa zima anapotekeleza wajibu wake wa kuwaongoza Watu wa Mungu na Ulimwengu katika ujumla wake, daima akitafuta kudumisha na kuimarisha misingi ya haki na amani.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, huduma ya upendo ni asili, utume na utambulisho wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee, Kanisa la Roma, ambalo kimsingi ni kielelezo cha upendo. Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali anahitimisha mahubiri yake kwa kuwaalika waamini kusali kwa ajili ya kuombea mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya, atakayetekeleza utume huu nyeti katika Kanisa.

Jiografia ya Makardinali wanaoingia kwenye Conclave mjini Vatican




Wakati huu wa uchaguzi wa Papa Mpya jambo la msingi kukumbuka ni kwamba, Kanisa ni moja, Takatifu, Katoliki, na la Mitume. Makardinali katika mwelekeo wa mawazo yao ya jumla wamebainisha kwamba, wanataka kumchagua Kiongozi mkuu wa Kanisa atakayeliongoza Kanisa la Kristo kama Baba mwenye huruma na mapendo, kielelezo cha umoja na mshikamano wa Kanisa; kiongozi mwenye dhamana ya kulinda na kusimamia kweli za Kiinjili, Maadili na utu wema. Haijalishi mahali anapotoka mtu, jambo la msingi ni kiongozi.

Kwa jumla, kuna Makardinali 115 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura wanaoanza mchakato huu kwenye Kikanisa cha Sistina kwa kula kiapo, tafakari ya Neno la Mungu na uchaguzi wa kwanza. Makardinali 60 wanatoka katika nchi za Ulaya, kuna Makardinali 33 kutoka Amerika, Makardinali 11 kutoka Barani Afrika, Asia kuna Makardinali 10 na Oceania kuna Kardinali mmoja. Itakumbukwa kwamba, kwenye Conclave ya Mwaka 2005, Kenya haikuwa na Kardinali, lakini mwaka huu, Kardinali John Njue yupo.

Kuna Makardinali 40 ambao wametekeleza utume wao au bado wanaendelea kufanya shughuli mbali mbali mjini Vatican. Kati ya Makardinali wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura 67 ni wale walioteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Wastani wa umri wa Makardinali wanaopiga kura ni kati ya miaka 71. Kardinali Walter Kasper mwenye umri wa miaka 80 ni kati ya wale waliobahatika kuingia katika Conclave wakiwa na umri mkubwa zaidi. Kati ya Makardinali vijana wana umri wa miaka 54 na 56. Kardinali Luis Antonio Tagle ana umri wa miaka 56.

Mwishoni, itakumbukwa kwamba, kundi la Makardinali Maaskofu lina Makardinali 6; Kundi la Makardinali Mapatriaki lina jumla ya Makardinali 4; Kundi la Makardinali Mapadre lina jumla ya Makardinali 153 na Makardinali Mashemasi wako 44. Kuna jumla ya Makardinali 207.

Shirikisha Invia articolo