Translate

Sunday, October 2, 2011

wanafunzi wa kike mbarali wahofiwa kubakwa

Na Thompson Mpanji,Mbarali

WANAFUNZI wa Kata ya Mahongole na Mwatenga,wilayani Mbarali wameuomba uongozi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuchukuwa jitihada za dhati kuwasaidia kuwajengea shule za Sekondari maeneo ya jirani  na makazi yao  ili kuepusha  madhara yanayoweza kuwakumba hasa kwa wanafunzi wa kike kutokana na kutembea  umbali mrefu katika vichaka   zaidi ya  kilomita 14  hadi kufikia shuleni.

Mwito huo umetolewa na wanafunzi hao walipokuwa wakizungumza na gazeti hili  kwa nyakati tofauti katika vijiji vya Kata  hizo ambapo wanafunzi kutoka Kijiji cha Sonyanga  wanatembea umbali wa kilomita zaidi ya nane hadi shule ya sekondari ya Kata ya Ruiwa,Ilongo  zaidi ya Kilimota 10,Kapyo umbali wa zaidi ya kilimota 14,Igalako na Mahongole Kilomita zaidi ya tatu,Muwela kilomita zaidi ya  saba na Mwatenga umbali wa kilomita zaidi ya 10.

Wanafunzi hao walisema, wamekuwa wakichoka na kushindwa kumsikiliza mwalimu  vyema baada ya kutemebea umbali mrefu ,wanafunzi wa kike wamekuwa wakihofiwa kubakwa vichakani huku wengine wakielelezea hofu yao ya kuuawa kutokana na  kuibuka kwa   matukio ya mauaji  ya kushtukiza  na kutulia yanayokuwa yakitokea wilayani humo jambo  ambalo wamedai linawakosesha raha na mori wa kuendelea na masomo.

Ofisa Mtendaji  Kata ya Mahongole,Juma Mangula  amethibitisha kuwepo kwa matatizo hayo kutokana na wanafunzi wa Kata ya Mahongole na Mwantenga kutegemea shule ya Sekondari ya Kata ya Ruiwa ambayo awali ilijengwa wakati wa Kata moja lakini  kwa sasa kuna uhitaji mkubwa wa shule.

Mangula alisema jitihada zinafanyika za kujenga mabweni ya wanafunzi wa kike ili kujaribu  kupunguza tatizo hilo na ameishukuru radio five kutembelea maeneo hayo ambayo  amedai hayajawahi kufikiwa na vyombo vya habari na ameviomba vyombo vingine kuiga mfano wa kituo cha radio five.

 Naye Diwani wa Kata ya Mahongole,Brown Mwakibete ametoa mwito kwa wadau  wa elimu kujitokeza kusaidia tatizo la shule kwani wananchi wamekuwa wakisua sua  kutokana na kutumia gharama nyingi na kwa muda mrefu katika kujenga  shule ya Sekondari ya Ruiwa ambayo kutokana na majengo yake kutokuwa na  ubora yameanguka na hivyo  kuanza kujenga shule nyingine.

Diwani Mwakibete alisema wakati wananchi wakiwa bado wanajitolea michango katika shule ya Sekondari ya Ruiwa  ikiwa na vyumba vya madarasa kumi na mbili,mabweni mawili,maktaba  na maabara ghafla ilibomoka na hivyo  wamechukua hatua ya kujenga shule mpya inayotegemewa na Kata ya Mahongole  na Mwantenga ambayo hadi sasa  ina vyumba 14 vya madarasa na nyumba mbili za walimu na kwamba bado haikidhi uhitaji wa wananchi wa kata hizo mbili

Mwisho

matukio ya nondo Mbeya,wauzaji na wamiliki wa bucha za nyama ya ng'ombe wadai mauzo yameshuka kutokana na walaji kuona kinyaa na kuichukia nyama,wasema wanaambulia kuuza maini na figo zisizotundikwa katika nondo

Na Thompson Mpanji,Mbeya

WAKATI matukio ya upigaji wa nondo yakiendelea kushika kasi jijini Mbeya,baadhi ya  wamiliki na wauza Bucha za  nyama ya Ng’ombe,jijini Mbeya wameelezea masikitiko yao ya kushuka kwa  mauzo ya nyama hiyo kutokana na walaji walio wengi  kuona kinyaa  na kuichukia nyama baada ya kuibuka kwa wimbi la uhalifu wa upigaji wa nondo unaohusishwa na imani za kishirikina kuwa zinatumika kuvuta wateja baada ya kutundikia nyama hizo katika maduka hayo.

Kama methali isemayo kufa kufaana ndivyo ilivyotokea kwa biashara hiyo ambapo kwa sasa wafanyabishara wa samaki, maharage,mboga za majani na nyinginezo nyota yao imenga’ra   kutokana na  wateja walio wengi  kuonekana wakikimbilia bidhaa hizo badala ya kitoweo maarufu cha  fileti,steki,mchanganyiko na mbavu.

Wakizungumza na mwamdishi wa habari hizi,  kwa nyakati tofauti,baadhi ya wauzaji na wamiliki wa mabucha  katika maeneo ya Soweto,Mabatini,Mwenjelwa,Mafiati na Sokomatola wamesema mauzo ya nyama hiyo yameporomoka kwa kasi  tangu kuibuka kwa  wimbi la upigaji wa nondo katika kipindi cha miezi kadhaa sasa.

Mmoja wa wauzaji wa Bucha eneo la Sokomatola aliyejimbaulisha kwa jina la Hussein  alisema kuwa nyama nyingi inalala kutokana na wateja kutoonekana  na kwamba wale wanaofika katika mabucha wananua  nyama aina ya figo au  maini ambazo hazitundikwi katika nondo.

Wakati huo huo,baadhi ya wakazi wa Kata ya Mabatini wamelalamikia Operesheni iliyofanywa na Jeshi la polisi kuwa imewaletea usumbufu mkubwa na kuwatia hasara baadhi ya wafanyabiashara kutokana na kikosi cha askari Polisi  kuvamia maeneo  hayo na kuwapiga marufuku wananchi kutembea kuanzia majira ya saa 1.30 usiku.

Mwenyekiti wa mtaa wa Mianzini,Kata ya Mabatini,Bibi.Elizabeth Mwambungu alisema operesheni iliyoendeshwa jana haikuwa ya kiistaarabu bali walitumia nguvu zaidi  kutokana na watu kupata usumbufu mkubwa wa kukamatwa na kupigwa ovyo jambo lililowafanya wajione kama wakimbizi ndani ya nchi yao.

Bibi.Mwambungu alisema kuwa  hawakuona umuhimu wa Jeshi hilo kufanya doria majira ya saa moja usiku huku muda wa watu kupigwa nondo unaonesha ni kuanzia saa 4 za usiku na kuendelea na kwamba wameshangazwa polisi kuanza doria baada ya kupigwa na kuuawa kwa askari mwenzao  huku  taarifa za upigwaji wa nondo zikifichwa na kudai kuwa  watu wanajeruhiwa ama kuuawa na vitu vyenye ncha kali.

Mwenyekiti huyo alisema uongozi wa mtaa wa mianzini umepanga kuitisha mkutano wa hadhara  siku ya Alhamis saa 8 mchana  kuzungumzia masuala ya ulinzi na usalama katika maeneo yao kufuatia kuibuka kwa vitendo vya upigaji wa nondo katika Kata ya Mbalizi Road ambapo imedaiwa  zaidi ya watu  9 wamejeruhiwa akiwepo mtu mmoja kuuawa.

Mchungaji Wiliam Mwamalanga akizungumza na gazeti hili alisema Kamanda wa polisi Mkoa wa Mbeya,Advocate Nyombi anapaswa kukubaliana na matokeo ya kuwa uhalifu wa upigaji wa nondo upo mkoani Mbeya na kwamba kilicho mbele yake ni kuweka mikakati kwa kushirikiana na wananchi kupambana na uhalifu huo kwa kutumia mbinu zilizotumika na Makamanda wenzake wa Mkoa wa Mbeya  waliopita  akitolea mfano Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Said Mwema na Alhaji Suleiman Kova waliofanikiwa kuzima kabisa kadhia hiyo.

Hata hivyo kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya kikao cha dharula cha Kata ya Mbalizi Road kilichoitishwajana  kufuatia matukio ya upigaji wa nondo katika eneo hilo usiku wa kuamkia  jana, imedaiwa kuwa mtu mmoja ameuawa na wengine saba  kujeruhiwa katika  Kata hiyo   wakiwepo wengine wawili  kutoka Kata ya Forest,zote za jijini hapa.

Mwisho.