Na Thompson Mpanji,Mbeya
WAKATI matukio ya upigaji wa
nondo yakiendelea kushika kasi jijini Mbeya,baadhi ya wamiliki na wauza Bucha za nyama ya Ng’ombe,jijini Mbeya wameelezea
masikitiko yao ya kushuka kwa mauzo ya
nyama hiyo kutokana na walaji walio wengi
kuona kinyaa na kuichukia nyama
baada ya kuibuka kwa wimbi la uhalifu wa upigaji wa nondo unaohusishwa na imani
za kishirikina kuwa zinatumika kuvuta wateja baada ya kutundikia nyama hizo
katika maduka hayo.
Kama methali isemayo kufa
kufaana ndivyo ilivyotokea kwa biashara hiyo ambapo kwa sasa wafanyabishara wa
samaki, maharage,mboga za majani na nyinginezo nyota yao imenga’ra kutokana na
wateja walio wengi kuonekana
wakikimbilia bidhaa hizo badala ya kitoweo maarufu cha fileti,steki,mchanganyiko na mbavu.
Wakizungumza na mwamdishi wa habari hizi, kwa nyakati tofauti,baadhi ya wauzaji na
wamiliki wa mabucha katika maeneo ya Soweto,Mabatini,Mwenjelwa,Mafiati na Sokomatola wamesema mauzo ya nyama hiyo
yameporomoka kwa kasi tangu kuibuka
kwa wimbi la upigaji wa nondo katika
kipindi cha miezi kadhaa sasa.
Mmoja wa wauzaji wa Bucha
eneo la Sokomatola aliyejimbaulisha kwa jina la Hussein alisema kuwa nyama nyingi inalala kutokana na
wateja kutoonekana na kwamba wale
wanaofika katika mabucha wananua nyama
aina ya figo au maini ambazo hazitundikwi
katika nondo.
Wakati huo huo,baadhi
ya wakazi wa Kata ya Mabatini wamelalamikia Operesheni iliyofanywa na Jeshi la
polisi kuwa imewaletea usumbufu mkubwa na kuwatia hasara baadhi ya
wafanyabiashara kutokana na kikosi cha askari Polisi kuvamia maeneo hayo na kuwapiga marufuku wananchi kutembea
kuanzia majira ya saa 1.30 usiku.
Mwenyekiti wa mtaa wa
Mianzini,Kata ya Mabatini,Bibi.Elizabeth Mwambungu alisema operesheni
iliyoendeshwa jana haikuwa ya kiistaarabu bali walitumia nguvu zaidi kutokana na watu kupata usumbufu mkubwa wa
kukamatwa na kupigwa ovyo jambo lililowafanya wajione kama wakimbizi ndani ya
nchi yao.
Bibi.Mwambungu alisema
kuwa hawakuona umuhimu wa Jeshi hilo
kufanya doria majira ya saa moja usiku huku muda wa watu kupigwa nondo
unaonesha ni kuanzia saa 4 za usiku na kuendelea na kwamba wameshangazwa polisi
kuanza doria baada ya kupigwa na kuuawa kwa askari mwenzao huku
taarifa za upigwaji wa nondo zikifichwa na kudai kuwa watu wanajeruhiwa ama kuuawa na vitu vyenye
ncha kali.
Mwenyekiti huyo alisema
uongozi wa mtaa wa mianzini umepanga kuitisha mkutano wa hadhara siku ya Alhamis saa 8 mchana kuzungumzia masuala ya ulinzi na usalama
katika maeneo yao kufuatia kuibuka kwa vitendo vya upigaji wa nondo katika Kata
ya Mbalizi Road ambapo imedaiwa zaidi ya
watu 9 wamejeruhiwa akiwepo mtu mmoja
kuuawa.
Mchungaji Wiliam Mwamalanga
akizungumza na gazeti hili alisema Kamanda wa polisi Mkoa wa Mbeya,Advocate
Nyombi anapaswa kukubaliana na matokeo ya kuwa uhalifu wa upigaji wa nondo upo
mkoani Mbeya na kwamba kilicho mbele yake ni kuweka mikakati kwa kushirikiana
na wananchi kupambana na uhalifu huo kwa kutumia mbinu zilizotumika na
Makamanda wenzake wa Mkoa wa Mbeya
waliopita akitolea mfano Mkuu wa
Jeshi la Polisi nchini, IGP Said Mwema na Alhaji Suleiman Kova waliofanikiwa
kuzima kabisa kadhia hiyo.
Hata hivyo kwa mujibu wa
taarifa kutoka ndani ya kikao cha dharula cha Kata ya Mbalizi Road
kilichoitishwajana kufuatia matukio ya
upigaji wa nondo katika eneo hilo usiku wa kuamkia jana, imedaiwa kuwa mtu mmoja ameuawa na
wengine saba kujeruhiwa katika Kata hiyo
wakiwepo wengine wawili kutoka
Kata ya Forest,zote za jijini hapa.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment