Maoni ya tume ya haki na amani
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
kuhusu rasimu ya Katiba Mpya
Yafuatayo ni maoni ya jumla ya rasimu ya Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania yaliyotolewa na Tume ya Haki na Amani Baraza la
Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Chama cha Wanataaluma Wakristo Tanzania,
CPT.
A: Utangulizi
Rasimu Na. 2 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitolewa na
kuwasilishwa rasmi kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete tarehe 30 Desemba, 2013.
Inawezekana kwamba, hadi sasa, si wote tumepata fursa ya kuipitia angalau mara
moja Rasimu hiyo. Nia ya andiko hili ni kutoa maoni ya jumla juu yake. Maoni
haya yameandaliwa na Sekretariati ya Tume ya Haki na Amani ya TEC kwa
kuzingatia tafakari na uchambuzi makini uliofanywa na Christian Professionals
of Tanzania (CPT).
B: Tuliyohimiza, Kuonya na Kutahadharisha Mwanzoni na Juu ya Rasimu Na. 1
Katika mapendekezo yetu ya mwanzo kabisa na yale juu ya Rasimu Na. 1,
tulihimiza, kusisitiza, na wakati mwingine kuonya na kutahadharisha
kiunyenyekevu lakini kwa makini na ufasaha wa maelezo, mambo muhimi yafuatayo,
kati ya mengine:
Misingi thabiti na halali ya Katiba
Mpya sharti iwe ni watu/utu, uhuru, haki, ukweli/uwazi na mshikamano
vinavyojenga hali ya amani na maendeleo yao/yake: Wananchi kuwa na haki na
uwezo zaidi wa kushiriki katika mambo ya maendeleo, uchumi na ya utawala wa
nchi yao kihalisia moja kwa moja na kwa njia za uwakilishi.
Umuhimu wa masharti ya kikatiba juu ya maadili mema, uwajibikaji, uwajibishwaji
na miiko ya viongozi na watumishi wa umma vikiendana na chombo (Tume) au
maelekezo na masharti muafaka ya utekelezaji wake kwa mujibu wa sheria
inayozingatia masharti ya Katiba Mpya.
Umuhimu wa umoja wa Taifa letu na uzalendo katika uongozi na utumishi wa umma
kwa lengo la kutumikia vyema wananchi na nchi (vizazi vya sasa na vijavyo) kwa
ujumla: Sera, malengo, mipango na sheria za Jamhuri ya Muungano na za Nchi
Washirika kutakiwa na Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano kuzingatia maslahi ya
nchi na wananchi walio wengi na hasa wale walio katika hali hatarishi ya
umaskini uliokithiri na jumuiya/makundi yenye vipato vya chini na kufuata
katika utekelezaji wake maelekezo na masharti ya Katiba hiyo ya Jamhuri ya
Muungano.
Umuhimu wa haki za binadamu zilizopanuliwa na kuboreshwa kwa kuzingatia maadili
mema na bila kukiuka sheria ya kimaumbile, ambazo yapasa zitekelezeke pasipo
mikwara ya kisheria inayokinzana na nia na madhumuni msingi ya Katiba na
inayoacha mianya ya dola/uongozi kukwepa uwajibikaji na uwajibishaji; umuhimu
wa kuimarisha haki ya mtu kuishi tangu kutungwa mimba, masharti ya kufuata na
kuendesha mambo ya kiimani/kidini pasipo kutumia njia hasi dhidi ya imani/dini
za wengine; nk.
Umuhimu wa Katiba Mpya kukomesha tatizo la Katiba na sheria kutoa kwa viongozi
na watumishi wakuu Serikalini mamlaka yasiyo na misingi, vigezo, taratibu wala
mipaka ungozi na muafaka ya kufuata katika utekelezaji wake au kutunga
sheria/kanuni za kuelekeza na kuongoza utekelezaji huo.
Katiba Mpya kudhibiti mamlaka na madaraka (yasiyo na vigezo, taratibu wala
kikomo katika utekelezaji wake isipokuwa busara na hekima kama sio hurka) ya
Rais: Kwamba katika kutekeleza madaraka hasa ya kuteua na kuwajibisha kinidhamu
viongozi wa juu Serikalini na katika utumishi wa umma, hatua za awali
zichukuliwe na kukamilishwa na vyombo wakilishi na shirikishi vya umma
vilivyoundwa na vinavyofanya kazi kwa mujibu wa ama Katiba Mpya au sheria
inayotimiza maelekezo na masharti ya Katiba hiyo – likiwemo Bunge. Kazi ya Rais
iwe ni kurasimisha yaliyofanywa na vyombo hivyo husika kwa misingi bora
kimaadili.
Kwamba Idara ya Mahakama iwe na haki ya kuwasilisha makadirio yake ya mapato na
matumizi ya mwaka moja kwa moja Bungeni kama Mhimili unaojisimamia ili
kuimarisha uhuru wake, hadhi yake na utawala wa kisheria nchini; na utaratibu
wa kuteua majaji na viongozi katika Mhimili huu ufuate mapendekezo kwenye kifungu
cha 6 hapo juu.
Kwamba na maeneo mengine ya utumishi wa umma kama Bunge, ulinzi na usalama,
polisi, utawala, maadili na uwajibikaji wa uongozi na watumishi wa umma,
usimamizi na uhakiki/udhibiti wa fedha za umma na mambo ya vyama vya siasa
yawekewe utaratibu wa kifetha na kuteua viongozi na watumishi waandamizi wake
unaofanana na ule unaotajwa kwenye kifungu cha 7 hapo juu.
Tangu mwanzo, suala la Muungano tulilichukulia msimamo wenye mambo ya kimsingi
matatu :
Muungano wetu una mizizi mirefu ya
kihistoria - kijamii, kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni -ikiwemo miaka hamsini
(50) ya Jamhuri ya Muungano pamoja na magumu na changamoto zake kubwa na ndogo.
Umuhimu wa kuzingatia ukweli kwamba wananchi wengi wa Bara na Zanzibar-Pemba ni
maskini au wa kipato duni kisichokidhi mahitaji. Hivyo, wanachohitaji ni
maendeleo kutokana na rasilmali ya sehemu hizi mbili, nyingi zikiwa Bara:
Muungano sharti ulenge kuleta maendeleo yao na Taifa, si kuwapa wachache
(watumishi wao) madaraka na uhondo wa uhuru; sharti uwe ni wa manufaa kubwa kwa
maendeleo ya Wananchi wote wa enzi hizi na wa nyakati na vizazi vijavyo.
(i) Muungano wa aina ya serikali mbili umeghubikwa na matatizo mengi ambayo
hayajawahi kujadiliwa na kutatuliwa kwa njia halisi na muafaka za kidemokrasia:
Lakini hiyo si sababu ya kutamani kurudi nyuma bali ni sababu ya kupiga moyo
konde na kutafuta suluhu inayoimarisha, siyo inayoyumbisha, Muungano katika
misingi yake ya ‘umoja ni nguvu utengano ni udhaifu’;
(ii) Dhana ya ‘Serkali tatu’ tangu mwanzo ilionekana haifai kwa sababu ya
gharama, udogo wa mmoja wa nchi Washirika, na sababu hii ya pili, pia, ilifanya
dhana ya ‘Serikali moja’ isitumike kwa hofu ya nchi hiyo ndogo kumezwa; na
(iii) CPT na Kanisa zima (kupitia TEC) mwanzoni tulipendekeza dhana ya ‘Serikali
moja’ kwa njia ya mchakato endelevu wa mjadala na maafikiano juu ya mambo
muhimu ya Muungano usio na kikomo cha muda bali wenye nia thabiti na lengo
mahsusi la umoja kwa misingi muafaka ya kidemokrasia. Hivyo, muundo wa Serikali
mbili ungeendelea kurekebishwa huku, pia, mambo ya Muungano yakiendelea
kuongezwa au kuboreshwa kwa nia na misingi hiyo. Ingawa kwenye mapendekezo yetu
(CPT-TEC) juu ya Rasimu Na. 1 tulitoa mawazo yetu juu ya muundo uliopendekezwa
na Tume ya Kurekebisha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuliendelea kuonya na kusisitiza juu
ya athari mbaya za muundo huo kwa mustakabali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Umuhimu wa Serikali kuwa ya
kisekula (kutokuwa na dini teule) au kuruhusu masuala ya kidini katika utawala
wa nchi (Jamhuri ya Muungano na Nchi Washirika); kutoruhusu mahusiano na nchi
nyingine au taasisi kama OIC yanayoilazimu
nchi au Serikali yetu kuvunja kanuni msingi hii ya usekula.
C: Ulinganisho kati ya Tuliyohimiza, kuonya na kutahadharisha na Maudhui ya
Rasimu Na. 2
Kwa kiwango kikubwa, mambo yaliyotajwa katika vipengele Na. 1 – 8 na 10
yamezingatiwa katika kuandaa Rasimu Na. 2, ingawa bado mtu angependa uboreshaji
wa hapa na pale. Lakini tunajua kuwa si kila tulilolipendekeza na hata kwa
msisitizo lingechukuliwa au kuwekwa kwa namna inayokithi matazamio na mapenzi
yetu; kwani pia yalikuwepo mapendekezo ya makundi na jumuiya nyingine ambazo
mawazo na mapendekezo yao ama yalikuwa yanafanana au yanatofautiana, au hata
kukinzana, na yale ya kwetu.
Tukipitia kila kipengele na kulinganisha tuliyopendekeza juu ya Rasimu Na. 1 na
yaliyomo katika Rasimu Na. 2 tutaona mara moja yaliyochukuliwa kwa namna moja
au nyingine hapa na pale na yaliyoachwa kabisa. Hapo, tujiulize ni yepi kati ya
yale yaliyoachwa kabisa yatupasa tuendelee kuyasisitiza na ni yepi tuyaache kwa
awamu hii ya mchakato wa kuunda Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mifano michache, kati ya masuala ambayo bado yanaibua maswali ndani ya
Wakatoliki na watu wengine wenye mwelelekeo wa mawazo unaofanana na wa Kanisa
Katoliki, ni kama ifuatavyo:
kulinda haki ya uhai tangu kutungwa
mimba kwa mtu;
kutajwa kwa “Mungu” angalau katika Utangulizi;
suala la mahusiano ya kimataifa kuwa ni sehemu ya mambo ya nchi za nje na hivyo
kuwa la Muungano na kupunguza uwezekano wa Nchi Washirika kuwa na mahusiano
yanayoweza kuimarisha utengano badala ya umoja hasa katika nyanja za kidini;
kukosa kanuni mahsusi ya kijumla ya kukomesha kikatiba tatizo la sheria na
kanuni nyingi zinazotoa madaraka yasiyo na mipaka na wajibu usio na masharti
fasaha na wazi ya taratibu, misingi, vigezo au adidu rejea na hatua za
kinidhamu za kuchukuliwa dhidi ya wasiowajibika na wasiowajibisha ipasavyo kwa
mujibu wa Katiba na/au sheria za nchi na, hivyo, kuacha mianya ya kukwepa
uwajibikaji na uwajibishaji wa viongozi, watumishi, mamlaka na vyombo vya umma.
Kama alivyoeleza Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Jaji Joseph S. Warioba, wakati akiwasilisha Rasimu Na.2, suala
lililoendelea kuitesa Tume hiyo hadi mwisho ni lile la Muungano. Sisi pia na
wengine wengi nchini lilitutesa na litaendelea kuibua hisia za mashaka: Picha
inayotoka ni kwamba moyo wa Watanzania wanaodaiwa na Tume kuwa pia ni wengi
kipindi hiki ni wa kuwa na muungano dhaifu wa aina ya Shirikisho si ya
kuimarisa na kuendeleza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa nchi huru mbili,
Tanganyika na Zanzibar, zilizojivua utaifa wa kila mojawapo ili kuunda Taifa
kubwa zaidi na lenye umoja, na hivyo, nguvu zaidi kuliko kila mojawapo ingebaki
katika hali yake ya awali ya utengano.
Huu, kama tulivyoonya na kutahadharisha awali,
ni moyo wa kuelekea kwenye kutengana si kuungana zaidi. Hapa, yatupasa
Watanzania wote tujiulize maswali yafuatayo na tuyatafakari kwa makini:
Je, Rasimu Na. 2 imejaribu vipi
kupunguza kasi ya kuporomoka kwa umoja wa kitaifa unaotegemezwa kwenye misingi
haba saba (7) iliyobaki?
Na je, yale yaliyopendekezwa yakipita vema kwenye mchakato wa ridhaa ya
Wananchi wa Tanzania
na kukubaliwa, mustakabali wa Muungano utasimama na kuhakikishwa kwa misingi
hiyo?
Au, je, kama baadaye Nchi Mshirika mojawapo ikitafuta uhuru zaidi kama si kujitoa kabisa katika Muungano, ile misingi
iliyobaki au itakayorekebishwa kukidhi ukiukwaji uliofanywa dhidi ya Katiba ya
sasa, itaweza kuhimili udidimiaji wa moyo wa kuuthamini umoja na kujenga hali
na mazingira ya uongozi na wananchi kuona hatari na hasara za utengano?
Je, tuko tayari kuona umoja wetu unasambaratika kama ilivyotokea na
inavyotishia kwingineko Barani Afrika [Sudan,
Ethiopia, DRC, Libya) na hata nje ya Afrika (USSR,Yugoslavia,
Czechoslavia, Muungano wa Kifalme wa Uingereza (UKoGB) ambako Scotland na North Ireland
zinatishia kujitenga na kuwa nchi huru kabisa, nk.]? Tutajiepushaje hali ya
kujikuta tunakabiliwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa sababu ya tabia na
mazoea hatarishi ya kutotumia njia adili za kuendesha masuala muhimu na nyeti
ya kitaifa likiwemo la Muungano?
Sababu zinazotolewa za kuendeleza
utengano zina asili gani, ya matakwa ya uhuru na maendeleo ya kweli ya wanyonge
au ya wenye (uchu na/au) malengo ya madaraka, maslahi binafsi na ya kitabaka
yanayokuzwa na kufanywa maslahi ya kitaifa na ya umma?
Je, katika Awamu hii ya IV ya utawala ndani ya Muungano, Muungano una mtetezi
katika Dola kati ya wale waliokula viapo kuulinda na kuutetea na, kama wapo, inakuwaje hatujawahi kuwaona au kuwasikia
wakijitokeza kidhati na kwa hoja makini -
kuutetea kwa hoja makini ya
kudhihirisha faida zake ambazo yapasa ziimarishwe, kulindwa na kuendelezwa kwa
manufaa na maslahi zaidi ya kizazi kilichopo na vijavyo?
kuhusu athari za kudhoofika na/au kuvunjika kwake kwa umma wa Watanzania wa
kizazi hiki na vizazi vijavyo?
Zinzoelezea jitihada na hatua thabiti na za dhati za kushughulikia mambo na
masuala ya Muungano kwa njia za kidemokrasia zilizo adili na makini, shirikishi
na wakilishi kwa ngazi za Wananchi na za Serikali?
Tume ya Jaji Warioba imeshindwa kujibu hoja yetu (CPT) ya kubainisha kiyakinifu
faida na athari za Muungano ambazo watu waliohojiwa walizitoa licha ya
kuorodhesha, pasipo ulinganifu na faida, kero zilizoelezewa (na wawakilishi?
wa) pande mbili (Nchi Washirika) za Muungano.
D: Yaliyo Bora na ya Kuhofia Kimaadili na kwa Mustakabali wa Umoja wa Kitaifa
Katika Rasimu N. 2
Ya Kuhofia Kimaadili na kwa Mustakabali wa Umoja wa Kitaifa
Kuna mambo matatu muhimu ya kutafakari pamoja kwa njia ya kujiuliza maswali
hasa baada ya kuyasikia na kuyasoma yaliyotolewa taarifa na yaliyopendekezwa na
Tume ya Kurekebisha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Tume ya Jaji
Warioba). Nayo ni kama ifuatavyo:-
Jambo la kwanza na kuu kati ya
mengineyo yanayotia wasiwasi kimaadili na ya kuhofia kwa mustakabali wa umoja
wa Taifa letu ni kwamba Tume ya Jaji Warioba imelazimika kupendekeza
mfumo/muundo wa Muungano wa serikali tatu badala ya mwendelezo wa serikali
mbili kwa sababu hasa ya kuzingatia hali halisi ya sasa ndani ya Muungano:
Kwamba mojawapo ya Nchi Washirika (Zanzibar) iliishafanya mabadiliko ya Katiba
yake kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania vile kwamba
haiwezekani hata kufikiria kuendeleza mfumo wa sasa wa Muungano wa serikali
mbili ambao vilevile umenung’unikiwa kwa muda mrefu kutokana na kinachoitwa
“kero” nyingi za mfumo huo wa serikali mbili. Maana yake ni kwamba tunalazimika
kufumua muundo wa sasa pasipo Nchi Washirika kwa pamoja na kwa njia muafaka
kujiandaa na kukubaliana kwanza juu ya hatua hiyo kwa sababu mojawapo wa Nchi
Washirika imeishajichukulia madaraka tayari ya kuufitinisha na kuubatilisha kwa
kufanya mabadiko kadhaa makubwa katika Katiba yake kinyume cha masharti ya
Katiba kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyouweka muundo huo.
Hofu na wasiwasi unaojitokeza kihalali kabisa ni kama
bado kuna moyo thabiti wa kuendeleza Muungano! Je, kilichotokea kinaashiria kwa
upande wa uongozi wa Nchi Washirika zote mbili utamaduni wa dhamira na maadili
ya umoja au ya ulegevu na udhaifu wa moyo unaoleteleza utengano? Uongozi wa
Muungano unathamini na uko makini kwa kiwango gani kuhusu masuala muhimu na
nyeti ya kitaifa?
Jambo la pili la kuhofia kimaadili
na kwa mustakabali wa umoja wa Taifa letu linatokana na hilo la kwanza: Nalo ni
kama Muungano wa aina ya Shirikisho unaopendekezwa umewekewa misingi ya kutosha
katika Rasimu Na. 2 ya Katiba ya Jamhri ya Muungano ya kuhakikisha kwamba
kilichojiri kwa muundo wa sasa hakitajirudia chini ya mfumo huo unaopendekezwa?
Katika hali ya udhaifu wa dhamira na maadili ya umoja wa kitaifa kwa uongozi,
kitakachozuia utovu kwa Nchi Washirika au mojawapo kudiriki kwenda njia yake
machoni pa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ni nini? Rasimu ya Katiba Na.2
inajibu vipi swali hili na jibu hilo
linatosheleza kuondoa wasiwasi huo na hofu hiyo?
Jambo la tatu na la mwisho kwa mada
hii ni la Watanzania kujiuliza kama Katiba ya sasa au ile inayopendekezwa na
Tume katika Rasimu N. 2 na hata ya aina nyingine yoyote ile tunayoweza kuibuka
nayo mwishoni mwa mchakato wa sasa wa kuunda Katiba Mpya inaweza kujibu na
kukidhi mahitaji, matakwa na matumaini yetu yote ya kikatiba? Je, tunaweza
kufikia hatua ya kusema kwa pamoja kama
Wananchi na Taifa bila kuwa na ngawanyiko wowote kwamba sasa tunayo Rasimu ya
Katiba aina ya mfano bora kuliko zote na ambayo ni muafaka kwa kila mmoja wetu
katika Nchi Washirika? Je, kuna nchi yoyote duniani ambayo ina katiba kama hiyo?
Je, mjadala juu ya ni kipi kilicho bora kwa wananchi na nchi leo na baadaye
kikatiba unaweza kufikia kikoma au ukamilifu au kusitishwa na nguvu yoyote ya
kimaumbile? Je, hofu na wasi wasi wetu wa sasa kimaadili na kwa mustakabali wa
umoja wa Taifa letu iwe ni sababu ya kutopokea kwa moyo mkunjufu kile
kinachoweza kunusuru dhamira na maadili ya umoja katika hali iliyobadilika
kihalisia?
Mlolongo huu wa maswali unadai sehemu ya majibu na ni hiyo tunayogeukia hapo
chini. Lakini nia si kujibu kila mojawapo ya hayo maswali, kwani mengi
yanaonyesha mwelelekeo wa kutohitaji jibu mahsusi. Nia ni kuona kama Rasimu Na. 2 ina maudhui ya mambo bora yanayoweza
kuendeleza umoja, kuimarisha mahusiano, mshikamano na kuleta maendeleo kwa
wananchi ndani ya Shirikisho la Nchi Washirika.
Kama yapo, swali ni kama yanaweza kuboreshwa na hivyo kutuwezesha kama Taifa,
katika kipindi hiki kigumu cha majaribu, kuvuka au kuyakabili magumu hayo
kijasiri na hivyo kuendelea kukomaa zaidi kitaifa kutokana na mchakato endelevu
wa tafakari, mjadala na maamuzi muafaka ya kidemokrasia kila inapowezekana au
kuonekana ni bora kufanya hivyo kwa ajili ya maendeleo na amani ya wananchi na
nchi yetu.
Kuna busara kubwa na unabii katika usemi : ”Yaliyopita si ndwele; tugange
yajayo!” Tusije tukajitia hatiani kwa kosa la ‘kuifanya migumu mioyo yetu’ na
hivyo kushindwa kuzing’amua tunu zilizowasilishwa mbele yetu katika Rasimu Na.
2 pamoja na changamoto zake Rasimu hiyo.
Basi tuangalie kama Rasimu Na. 2 imetuwekea
misingi bora ya kuweza kuganga yajayo.
Yaliyo Bora Kimaadili na kwa Umoja wa Taifa
Yapo mambo kati ya maudhui ya Rasimu Na. 2 ambayo ni mazuri na muhimu kiasi
kwamba yapasa tuyachukulie kama mambo msingi yanayobeba na yanaweza kudumisha
na kuendeleza utamaduni, maadili na dhamira au moyo wa umoja wa nchi yetu
Tanzania katika hali halisi ya sasa. K`wayo, katika mazingira ya umoja wa aina
ya shirikisho, kuna uwezekano kwa Nchi Washirika (viongozi na wananchi wake) -
kuendeleza kidemokrasia mahusiano
ya karibu kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni na kwa kutambua mema ya kushirikiana
kwa namna hiyo zaidi na zaidi na magumu ya kufanya kinyume chake;
kutambua umuhimu wa kuheshimiana na kushirikiana kimshikamano kwa misingi iliyo
bora na iliyowekwa kikatiba kwa maridhiano muafaka; na
kutambua na kuthamini vema tunu na rasilmali za kila Nchi Mshirika zinazoweza
kutumika kwa manufaa zaidi kwa wananchi kwa kuongeza, kuimarisha na kuendeleza
zaidi misingi ya mshikamano na umoja kisiasa, kiuchumi na/au kiutamaduni.
Kwa ajili ya hayo, ni muhimu tutambue mambo manne ya msingi zaidi kijamii kwa
umoja wa Nchi Washirika katika aina yoyote ya muungano au mashikirikiano: Mambo
hayo hudhihirika katika kiwango cha juu cha kufanana na kuzingatiwa katika
nyanja nne (4) za maisha ya siku hadi siku. Na hayo mambo, pamoja na nyanja
hizo, ni kama ifuatavyo:
(a) Utamaduni (lugha, maadili, mila na desturi na historia ya pamoja ya
mahusiano/ushirikiano wenye manufaa kwa Nchi/Wananchi Wahusika);
(b) Mifumo ya kisheria (Katiba, sheria na kanuni msingi);
(c) Miundo ya dola (wizara, idara, taasisi na asasi zake kuu na za kijamii);
na, kubwa kuliko yote
(d) Moyo wa kuthamini umoja na ushirikiano kwa misingi thabiti na muafaka ya
‘toa na pokea’ (toa chako anachohitaji mwenzako ili nawe upokee chake
unachohitaji kwake), uhuru, haki, ukweli na mshikamano kwa misingi ya kuheshimiana
na kustahimiliana.
Mambo haya na nyanja hizi nne kati ya nyingine tukizitafakari na kuzijadili kwa
makini tutagundua siri ya udumifu wa umoja, ushirikiano na mshikamano wa dhati
wa madola, taasisi za kikanda na za kimataifa na hata kila dola na kila nchi
iliyo na sifa au historia inayoashiria uwepo wa mambo hayo. Nyanja hizi
zinawezesha mazungumzo na mjadala endelevu wa kuelekeza nchi ndogo au kubwa,
moja au mbili na hata zaidi kwenye namna moja ya umoja au ushirikiano kutoka
viwango vya chini hadi vya kileleni. Kwa uhakika, misingi hii hii inaendelea
kusaidia dunia kujenga hali mpya ya mahusiano na ushirikiano wa kikanda na wa
kimataifa pasipo wakati wote utumiaji wa mabavu, mauaji na maangamizi ya
kivita.
Kwa kuzingatia maelezo hayo, tuangalie kwa kifupi, mambo yaliyo bora katika
Rasimu Na. 2 yanayoweza kuwa ni nguzo za kuegemezea umoja na ushirikiano
endelevu chini ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nayo ni kama
ifuatavyo:
(1)Yale yote yaliyo kwenye Sura ya Kwanza hadi
Sura ya Nne; yaani:
Jina, Mipaka, Alama, Lugha na Tunu
za Taifa; Mamlaka ya Wananchi, Utii na Hifadhi ya Katiba;
Malengo Muhimu, Misingi ya Mwelekeo wa Shughuli za Serikali na Sera za Kitaifa;
Maadili na Miiko ya Uongozi na Utumishi wa Umma; na
Haki za Binadamu, Wajibu wa Raia na Mamlaka za Nchi (na Mipaka ya Haki za
Binadamu).
Kati ya hayo, yale yaliyo katika Sura ya Kwana, Sura ya Pili na Sura ya Nne ni
baadhi ya mambo sita (6) ambayo hayawezi kufanyiwa mabadiliko -
“hadi mabadiliko hayo yaungwe mkono na theruthi mbili ya wananchi wa Jamhuri ya
Muungano kutoka kila upande wa Jamhuri ya Muungano kwa Kura ya Maoni
itakayoendeshwa na kusimamiwa na Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa mujibu wa sheria za nchi”.
Masharti kuhusu Uraia wa Jamhuri ya
Muungano yanafanya jambo hilo
muhimu liwe na hadhi ya kikatiba, ambapo hadi sasa halikuwa la kikatiba bali la
sheria ya kawaida iliyotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano.
Masharti kuhusu Serikali ya Jamhuri ya Muungano - Serikali, Rais, Makamu wa
Rais na Baraza la Mawaziri pamoja na Tume ya Uhusiano na Uratibu wa Serikali
hiyo - licha ya kuwa lina magumu na changamoto kadhaa za ‘’Shirikisho’’, lina
uzuri wa kuendeleza dhana na siasa ya umoja na mshikamano wa kitaifa ndani ya
Jamhuri ya Muungano-Shirikisho wa (Nchi Washirika) Tanzania.
Bunge la Jamhuri ya Muungano ni jambo kubwa lingine la kutilia maanani kama chombo kimojawapo cha kusaidia kuendeleza mjadala,
mahusiano, sheria, kanuni na taratibu rasmi za umoja wa kitaifa katika hali
iliyobadilika kikatiba kwenye muundo wa dola la Taifa na kupungua kwa mambo ya
Muungano au umoja wa kitaifa.
Mahakama (ya Juu na ya Rufani) ya
Jamhuri ya Muungano itakuwa chombo muhimu sana
cha kujenga msingi mpya na kuimarisha misingi iliyodhoofishwa ya kisiasa,
kiutamaduni na hata ya kiuchumi ya Jamhuri ya Muungano-Shirikisho. Masharti
husika ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya sasa yanaunda Mahakama ya Jamhuri
isiyo na madaraka juu ya raia na dola ya kuamua mashauri na kuwajibisha bali ya
kushauri na kusuruhisha tu. Hata hivyo, hayajawahi kutekelezwa hadi leo.
Masharti ya Katiba tarajiwa kwa Mujibu wa Rasimu Na. 2, yanaifanya “Mahakama ya
Juu [kuwa] ni ngazi ya mwisho ya rufani katika Jamhuri ya Muungano ...”. Aidha,
inatoa kwa Mahakama ya Juu hiyo madaraka ya–
(a) pekee na ya awali ya kusikiliza na kuamua mashauri yanayohusu matokeo ya
uchaguzi wa Rais wa Jamhyri ya Muungano;
(b) kusikiliza na kuamua mashauri yatakayowasilishwa na wananchi, Serikali za
Nchi Washirika kuhusu tafsiri au utekelezaji wa Katiba hii;
(c)usikiliza na kuamua migogoro baina ya Nchi Washirika na Serikali ya Jamhuri
ya Muungano;
(d)kusikiliza na kuamua rufani kutoka Mahakama ya Rufani [ya Jamhuri ya
Muungano];
(e)kutoa ushauri kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali za Nchi
Washirika, pale itakapoombwa; na
(f)kusikiliza na kuamua shauri lolote litakalowasilishwa mbele yake kwa mujibu
wa Katiba hii au sheria nyingine yoyote itakayoipa Mahakama hiyo mamlaka.
Vile vile “Mahakama ya Rufani pamoja na mahakama za Nchi Washirka, isipokuwa
Mahakama ya Juu, zitalazimika kufuata maamuzi ya Mahakama ya Juu”.
Pamoja na hayo, Ibara ya 167(1) inaipa Mahakama ya Rufani mamlaka ya-
kusikiliza na kuamua kila rufani
inayowasilishwa mbele ya Mahakama ya Rufani kutokana na hukumu au uamuzi wowote
wa Mahakama Kuu za Nchi Washirika au Mahakama yoyote ya chini iliyopewa mamlaka
maalumu ya kusikiliza mashauri ambayo kwa kawaida husikilizwa na Mahakama Kuu;
kufanya mapitio ya maamuzi ya Mahakama Kuu za Nchi Washirika au mahakama yoyote
ya chini iliyopewa mamlaka kusikiliza mashauri ambayo kwa kawaida husikiliwa na
Mahakama Kuu.
Jambo la Ulinzi na Usalama wa
Jamhuri ya Muungano
Umuhimu wa jambo hili kwa kuendeleza umoja wa kitaifa katika hali iliyobadilika
ni mkubwa na wa kimsingi kabisa. Kwa mujibu wa Ibara ya 1 ya Rasimu Na. 2,
licha ya kwamba kinachopendekezwa ni Muungano wenye muundo wa Serikali Tatu,
bado umoja wa kitaifa kikatiba utabaki kama
hayo yote yaliyoelezwa tayari na yanayofuata hapa chini yanavyoashiria.
Tukianza na hiyo Ibara ya 1:
(1) Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
ni Nchi na Shirikisho lenye mamlaka kamili ambalo limetokana na Muungano wa nch
mbili za Jamhuri ya Tanganyika
na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar,
ambazo kabla ya Hati ya Makubaliano ya Muungano ya mwaka 1964, zilikuwa nchi
huru.
Aidha, chini ya Ibara ya 71 kuhusu Rais wa Jamhuri ya Muungano,
(2) Rais wa Jamhuri ya Muungano atakuwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na
Amiri Jeshi Mkuu na:
(a) atakuwa taswira ya Jamhuri ya Muungano na watu wake;
(b) atakuwa alama ya umoja, uhuru wa nchi na mamlaka yake; na
(c) atakuwa na dhamana ya kukuza na kuhifadhi umoja wa kitaifa.
Ibara ya 235(1) inatamka kuwa «jukumu la ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya
Muungano ni la kila rai». Hata hivyo, Ibara ya 236 inaweka masharti kuhusu
vyombo vya Ulini na Usalama wa Taifa:
Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania;
Jeshila Polisi la Jamhuri ya Muungano; na
Idara ya Usalama wa Taifa.
Chini ya Ibara ndogo ya 236(4) na (5):
Mtu hataruhusiwa kuanzisha taasisi, kampuni, jumuiya au shirika linalohusiana
na ulinzi na usalama wa Taifa au ushirika wa kijeshi, isipokuwa kama inavyoruhusiwa na Katiba hii au sheria za nchi.
Vyombo vya ulinzi na usalama wa Taifa vitakuwa chini ya mamlaka ya Rais.
Haya si mambo ya kubeza au kuchukuliwa kivyepesi bali kuyaona kuwa ni baadhi ya
misingi ya umoja wa Taifa letu kusimamia na kusonga mbele katika hali mpya
kikatiba, kisiasa na kiuchumi.
Jambo lingine bora ambalo ni kubwa
na la msingi kimaadili na kwa mustakabali wa umoja wa Taifa ni masharti
yanayohusu Tume (Huru), Mabaraza na Kamati mbalimbali zilizoundwa kikatiba kwa
ajili ya maeneo na sehemu zote muhimu za utumishi wa umma. Hivi ni vyombo
vyenye dhima ya kuweka kwa mujibu wa sheria misingi ya taratibu za uwazi, na
iliyo shirikishi na wakilishi katika uteuzi wa viongozi wa juu na watumishi waandamizi
wa umma na masuala husika ya kimaslahi na ya kinidhamu. Kwavyo, tatizo la
Mhimili mmoja wapo (Serikali/Urais) wa Mihimili mitatu ya Dola kuwa na madaraka
yasiyo na mipaka, misingi, vigezo na taratibu muafaka na wazi linaweza
kudhibitiwa kwa kiwango kikubwa.
Tume hizo muhimu kwa majina ni kama ifuatavyo:
Tume Huru ya Uchaguzi ya (Jamhuri
ya) Muungano;
Tume ya Uhusiano na Uratibu wa Serikali;
Tume ya Utumishi wa Bunge;
Tume ya Utumishi wa Mahakama;
Tume [Huru] ya Maadili na Uongozi na Uwajibikaji;
Tume [Huru] ya Haki za Binadamu;
Tume ya Utumishi ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania;
Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi.
Kamati za Muungano ni kama ifuatavyo:-
Kamati ya Uteuzi wa Mwenyekiti,
Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi;
Kamati Maalimu ya Uteuzi [wa Viongozi na Watumishi Waandamizi wa Umma];
Kamati Maalimu ya Uteuzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wa Tume
ya Haki za Binadamu;
Kamati ya Utekelezaji wa Katiba katika Muda wa Mpito.
Kuna Baraza moja la Muungano lililopendekezwa, nalo ni:
Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa.
Rasimu imependekeza miaka minne (4)
ya Kipindi cha Mpito. Mauthui ya Ibara husika ni mazuri na kwa kiwango kikubwa
yanakidhi mapendekezo yetu na bila shaka na ya watu na asasi nyinginezo zilizowasilisha
maoni kwa Tume ya Jaji Warioba. Kamati maalumu ya kusimamia na kuratibu
utekelezaji wa Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano inayopendekezwa, pia,
itashughulikia mapendekezo ya sheria muafaka mbalimbali zinazolengwa na Katiba
Mpya hiyo pamoja na urekebishaji wa sheria nyingine zitakazoathiriwa na Katiba
hiyo.
Kipindi hiki muhimu kitatoa fursa ya kwanza kwa Wananchi na viongozi wao
kujipanga upya baada ya Katiba Mpya kupitishwa kulingana na masharti ya Katiba
hiyo. Kitakuwa ni kipindi cha kuendelea kujadiliana, kutafautiana bila kuzozana
na kukubaliana kwa misingi ya kidemokrasia na katika hali ya amani na utuluvu.
Hii itatokea kama tutafanikiwa kukabili vema changamoto za mchakato kabla na
wakati wa kuijadili na kuipitisha Katiba Mpya tarajiwa katika hatua za awali
mbili zilizobaki, ya Baraza la Kutunga Katiba na Kura
ya Maoni. Hivyo, pia, utakuwa ni wakati muafaka wa kutahini moyo wetu wa umoja
na ukomavu wetu wa kisiasa kama Taifa.
TUOMBE MUNGU!
F: Hitimisho
Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 2013 ilitegemewa kuibua
mjadala wenye msisimko wa aina yake; kwani umechangiwa mawazo, maoni na hata
mapendekezo maalumu yaliyotolewa kwa mdomo, kwa maandishi na kwa njia nyingi
mbalimbali zilizokaribishwa na Tume ya Jaji Warioba. Jambo moja la wazi tangu
Rasimu Na. 1 kutangazwa ni la Wananchi kugawanyika katika makundi makuu manne.
Jambo hilo ni lile la muundo wa Jamhuri ya Muungano: Baadhi, wanapendelea
muundo wa sasa wa Serikali mbili uendelee; baadhi, ule wa Serikali moja (mara
moja, katika muda mfupi au, kimchakato, baada ya muda usiotabilika sasa),
baadhi, ule wa Serikali tatu, kama Rasimu inavyopendekeza, na baadhi, Muungano
wa mkataba. Haijulikani hatima ya mjadala huu kipindi hiki itakuwa nini au
vipi: Je tutaibuka na Katiba Mpya au tutarejea kwenye Katiba tata ya sasa?
Itakumbukwa kuwa tulijiuliza swali hili tangu mwanzo wa mchakato wa
kushughulikia suala la Katiba Mpya chini ya Sheria husika na ya Tume ya Jaji
Warioba; na bado linatukabili!
Lakini hali hii isitutishe wala kutupa wasiwasi kwani inaashiria jinsi watu
walivyoamka kisiasa na kwamba kweli wanataka mabadiliko. Hata hivyo, mabadiliko
hayo wanayotaka kwa dhati hayaashiriwi hasa na mawazo kuhusu muundo wa Serikali
ya Jamhuri ya Muungano. Kwa kuichambua Rasimu kwa makini tumeona kwamba yako
mambo yaliyo muhimu na ya msingi zaidi kimaadili na kwa maendeleo na
mustakabali wa Taifa letu katika hali ya umoja kuliko inavyoonekana kijuujuu.
Cha kuhofia ni kama katika Nchi Washirika kuna
moyo wa dhati wa umoja, hasa kwenye ngazi ya viongoi wa kisiasa, wa kuyathamini
hayo yaliyo muhimu na ya msingi zaidi na kukubali ‘tugange yajayo’. Kuwania
madaraka na umaarufu wa kisiasa, na hivyo, kuweka mkazo katika mambo ya
kimuundo na kuhofia mabadiliko ya kimsingi katika mgawanyo wa madaraka ya
kiutawala kunaweza kuteka mjadala na mchakato mzima. Hivyo, tusipokuwa makini,
tunaweza kuingizwa au kujikuta tumesukumizwa kwenye bwawa la tope la malumbano
na hoja zisizo na tija wala maslahi halisi kwa umma wa Wananchi pande zote
mbili za Muungano.
Je, CPT na Mama Kanisa Katoloki chini ya TEC kwa ujumla wetu tuko tayari
kusimama, kuungana na wengine wenye mapenzi mema na kutetea yote yaliyo bora,
kushauri namna ya kushughulikia yanayotia hofu kwa njia adili na kuhadharisha
umma, kukemea na kuonya, panapolazimu, kiadilifu? Wanaotaka kujenga nguvu ya
hoja na sio hoja ya nguvu, tuwasikilize na tujadiliane pamoja kihoja.
Wale watakaoendekeza hoja ya nguvu, ya kulazimisha kimabavu, tuwakemee na
kuwaonya ipasavyo kihoja vivile na kwa unyenyekevu wa moyo. Nyakati hizi ni za
demokrasia, uwazi, kujenga mshikamano kwa ridhaa ya wenye mamlaka na Wananchi
katika Nchi Washirika zote mbili kwa busara, hekima, unyenyekevu na
ustahimilivu wa moyo mpana.
Kwa vyovyote vile na kama alivyoasa Mwadhama Policarp Kardinali Pengo kwenye
mkutano wa Hija wa WAWATA majuzi, yatupasa tusali na kuomba Mungu atuepushe na
janga linaloweza kutokea kutokana na kutengana kwa shari na chuki kwa
kinachoitwa “kero za Muungano za muda mrefu”.
Tusisahau tahadhari na maonyo ya Hayati Baba wa Taifa, Julius K. Nyerere
anayebezwa na kudhihakiwa na maadui wa umoja wa Jamhuri ya Muungano kwa maneno
makali na mengi ya uzushi na ya kashfa. Aliyosema ni ya kinabii: dhambi ya
kubaguana kwa misingi ya Utanganyika na/au Uzanzibari inaweza kuzaa balaa la
wananchi na uongozi baguzi kubaguana ndani kwa ndani ya Nchi Washirika au Nchi
Mshirika itakayoitenda dhambi hiyo kwa hasara na madhara kwa wote, Wananchi na
Nchi Washirika. Hivyo, hata kama mtenda dhambi
hiyo ni mojawapo ya hizo Nchi Washirika, madhara yake yataathiri vibaya Nchi
Washirika zote mbili kutokana na jinsi zilivyo kijamii!