Translate

Monday, December 24, 2012

watoto waandikishwa kwa malipo Mbeya

Na Thompson Mpanji,Mbeya
 
BAADHI ya wazazi jijini hapa wamelalamikia hatua ya serikali ya mtaa wa Ilomba,jijini Mbeya kuwatoza Sh.12,500 mchango wa kuandikisha jina  la kuingia darasa la kwanza mwaka 2013.
 
Hatua hiyo inadaiwa kwenda kinyume na maagizo ya Waziri wa nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI),Kassim majaliwa kuwa kuandikisha darasa la kwanza ni bure na hakuna michango yeyote iliyoruhusiwa kisheria.
 
Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya wazazi (majina yamehifadhiwa)walisema kuwa wameshangazwa  viongozi wa serikali ya mtaa kuandikisha majina ya watoto kwa kutoza sh.12,500 na kwamba mzazi asiyekuwa na kiasi hicho mtoto wake hawezi kupokelewa.
 
Walisema wameambiwa kuwa mzazi ambaye hataweza kutoa fedha hiyo mtoto wake hawezi kusoma shuleni hapo na endapo atakubaliwa basi atatakiwa kukaa chini kwenye vumbi hatoruhusiwa kukalia dawati jambo ambalo wamedai ni unyanyasaji.
 
"Wametuambia eti kama hatutowi basi watoto wetu watakuwa wakisoma huku wakiwa wamekaa kwenye vumbi darasani na wenzao waliolipa watakaa katika madawati…ndiyo maana watoto wetu wanarudi wamechafuka ovyo kila siku kumbe ni sababu ya kuwanyanyapaa,"alisema.
 
Mmoja wa wajumbe wa serikali ya mtaa wa Ilomba,Mwl.Edwin Kamweli alisema hizo ni mbinu chafu za baadhi ya wanasiasa kutaka kuzorotesha maendeleo ya mtaa wa Ilomba kwani mkutano wa hadhara ulikaa na kukubaliana wanannchi wote kutoa mchango huo kwa ajili ya kuboresha mazingira ya shule.
 
"Huu mfumo wa vyama vingi utaturudisha nyuma tukiendekeza maneno bila vitendo…kuna watu wavivu wanatumia fursa ya demokrasia kuturudisha nyuma na sisi tunasema hatuwezi kukubali na haiwasaiidii tunasonga mbele…vikao na mikutano ikiitishwa wanasema wapo bize tuikipitisha maazimio wanasema tunawaonea,"alisema.
 
Mwl.Kamwela alisema kiasi hicho cha sh.12,500 kilipitishwa na wananchi waliohudhuria mkutano mmoja wa hadhara ikiwa na lengo la kuboresha mazingira ya shule na wanafunzi ili waweze kusoma bila kubanana.
 
Alisema mgawanyo wa fedha hiyo ni Sh.10,000 kwa ajili ya dawati litakalochangiwa na wanafunzi watatu watakaolitumia ambapo kila mmoja atachangia kiasi hicho na kukamilisha gharama ya ununuzi wa dawati moja kwa Sh.30,000.
 
Mwalimu huyo mstaafu aliendelea kufafanua kuwa katika shule hizo mbili za Kagera na Ruanda Nzwovwe kuna mlinzi anayelipwa na hivyo kila mzazi wamekubaliana achangie Sh.1,500 ambapo mchango wa maji ni Sh.1,000.
 
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ilomba,Erasto Mwakapoma alifafanua kuwa uandikishwaji ni bure lakini michango hiyo ilitokana na wananchi wenyewe baada ya kukaa katika mkutano wa hadhara wa mtaa wa Ilomba Novemba,30,2012 ambapo yeye alikaribishwa na kwamba wanaochangia ni wananchi wote na siyo wazazi wanaowaandikisha watoto shule pekee.
 
Mwakapoma alisema shule ya smingi Kagera na Ruanda Nzovwe zinatarajia kuandikisha watoto zaidi ya 200 ingawa lengo lilikuwa watoto 130,lakini hawatoweza kukataa kuwaaandiskisha watoto waliofikia umri wa kwenda shule hivyo kunahitajika madawati ya ziada.
 
Mwisho.

No comments:

Post a Comment