Translate

Monday, December 24, 2012

Kanisa katoliki laishangaa Tanesco Mbeya kuwabambikia deni la zaidi ya Sh.Mil.20,

Na Thompson Mpanji,Mbeya
 
KANISA Katoliki Jimbo la Mbeya  limelishangaa Shirika la Umeme la Taifa (TANESCO)Mbeya kwa kuliamisha deni la umeme lenye thamani ya zaidi ya Sh.Mil.20 na kulibambikia kanisa,kukataa umeme kwa takribani mwezi mmoja sasa sanjari na kung’oa waya wa ‘service line’ na kusababisha ukosefu wa umeme kwa takribani mwezi mmoja tangu mwezi Novemba,2012.
 
Aidha kanisa hilo limesema limeshindwa kuelewa nia ya uongozi wa tanesco Mbeya kutokana na deni hilo huku wakiwa na majibu ya dharau, limemuomba Waziri wa Nishati na Madini Prof.Sospeter Muhungo kuingilia kati suala hilo na kulimaliza.
 
"Hatutaki kuingia zaidi kuhusina na suala hili…tunamsihi Waziri Muhongo aingilie kati suala hili hatupendi kufika mbali …afuatilie ataona mauza uza wanayoyafanya watumishi wake wa Tanesco ambao wanaona kama shirika ni mali yao na kumpatia mtu deni mtu ambalo siyo haki yake ni rahisi ,"alisema Mwenyekiti wa Halmashauri ya walei jimbo la Mbeya,Magoma.
 
Mwenyekiti huyo alisema alipokea malalamiko kutoka kwa wapangaji wa nyumba ambazo zinamilikiwa na kanisa Katoliki jimbo la Mbeya kuwa wamekatiwa umeme kwa kudaiwa deni la Sh.Mil.4 na baada ya kufuatilia walibadilishiwa na kuambiwa wanadaiwa Sh.Mil.16 na kwamba wamehamishiwa deni hilo katika mita yao ili watoe msukumo kwa kanisa kulilipa deni ambalo wamekuwa wakipiga chenga kulilipa.
 
Magoma alisema mazingira ya majibu hayo yanaonesha dhahiri kuwa baadhi ya watumishi wa Tanesco hawajatenda haki kwa kuhamishia deni katika akaunti ambayo haidaiwi,lakini bado amekuwa akijiuliza kama kanisa linadaiwa Tanesco Mbeya imeshindwa nini kufuatilia badala ya kwenda kuwabambikia deni la mamilioni watu ambao hawana uwezo wa kulilipa deni hilo hata baada ya miaka 100 kama siyo kuwadhulumu haki ya kupata umeme.
 
 
Bibi.Veronika Mwazembe Mkazi wa nyumba hizo kwa sasa Mtakatifu mathias Mulumba alisema wanao ushahidi wa kulipa deni la mita lililoachwa na watumiaji wengine iliyokuwa ikidaiwa tangu mwaka 2010 na kuthibitishwa na ofisa wa Tanesco Mbeya aliyesaini ambapo wamelilipa taratibu hadi kulimaliza.
 
Bibi.Mwazembe alisema baada ya kumaliza deni hilo mwaka 2011 walibadilishiwa mita ya luku na kuendelea kuitumia lakini katika hatua ya kushangaza oktoba,2012 wamezuiwa kutumia huduma hiyo kwa madai ya kudaiwa zaidi ya Sh.mil.16 jambo ambalo limewakatisha tamaa ya kuendelea kunufaika na umeme wa shirika la Tanesco kwa madai hata kama lingekuwa ni deni halali hawana uwezo wa kulilipa hata kwa miaka 100 ijayo.
 
Mkazi mwingine ambaye aliomba jina lake kuhifadhiwa kwa sababu maalum alisema wateja wa Tanesco wanaokutwa wameiba umeme kwa kujiunganishia isivyo halali wanachukuliwa hatua kali za kisheria hivyo kwanini shirika hilo nalo lisifikishwe mahakamani kwa kuwalimbikizia deni watu wasiohusika huku wakijuwa ni uonevu,unyanyasaji, kinyume na haki za binadamu sanjari na makosa kisheria.
 
Alisema baada ya kufungiwa kutumia umeme walifika kutoa malalamiko yao kwa Mhasibu wa Tanesco Mkoa aliyemtaja kwa jina moja la Mkotwe ambaye alidai ofisa aliyekuwa akishughulikia suala hilo yupo Dar es salaam kikazi kwa hiyo anawafungulia kwa muda kutumia umeme wakati wakiendelea kumsubiri mhusika kuja kutatua madai hayo ya deni la Sh.mil.4.
 
Alifafanua kuwa mwezi Novemba,2012 walipoenda kununua umeme wa Luku waliambiwa wamefungiwa na baada ya kuwasiliana na wahusika wa huduma kwa wateja wa Luku makao makuu Dar es salaama waliwaambia kuwa wanadaiwa Sh.mil.10 katika mita moja na Sh.mil.6 katika mita nyingine jambo ambalo liliwashtusha.
 
Mteja huyo alisema walishangazwa na taarifa hiyo ambayo awali mwezi oktoba ilionekana wanadaiwa Sh.Mil.4 ambazo ziliingizwa kimakosa na kwamba katika hatua ya kushangaza inaonesha dhahiri kuwa Mhasibu wa Tanesco mkoa alionesha deni la awali wateja wamelikubali na hivyo kukatwa asilimia 100 yaani asilimia 50 kwa mita moja na asilimia 50 kwa mita nyingine jambo lililowatia mashaka kuwa Mhasibu huyo anahusika na kuwahujumu.
 
Aidha alisema baada ya kuwasiliana na Mhasibu huyo aliwaambia baada ya kufungua katika mfumo wa awali na kubadilisha masharti, wateja hao wanatakiwa kulipia kiasi cha Sh.100,000 ama 500,000 kupunguza deni ili wafunguliwe umeme na kuendelea kuutumia.
 
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa kuna mchezo mchafu unaochezwa na baadhi ya maofisa wa Tanesco kubambika madeni watu wasiohusika ikiwa ni njia mojawapo ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu huku wakiwaacha walalahoi wakikosa matumaini na imani na shirika lao la kitanzania.
 
Gazeti hili liliwasiliana na Ofisa anayehusika na udhibiti wa madeni aliyejitambulisha kwa jina la Rehema ambaye alikiri kuwa deni hilo siyo la wahusika wanaotumia luku lakini kutokana na kanisa katoliki jimbo la Mbeya ambao wamenunua nyumba hizo kutoka kampuni ya Mbeya Retco kupuuzia kulilipa deni hilo wamefikia uamuzi wa kulihamishia katika mita ya luku inayotumiwa na wapangaji ambayo haikuwa na deni.
 
Ofisa huyo alisema wateja hao wanaolalamika wanapaswa kulishinikiza kanisa kulilipia deni hilo ili nao waendelee kupata huduma hiyo vinginevyo wataendelea kukosa huduma hiyo na kwamba hata kanisa likibomoa nyumba hizo na kujenga nyumba nyingine deni hilo litaendelea kuongezeka na watapaswa walilipe hata baada ya miaka 100.
 
Mmoja wa wafanyakazi wa Tanesco ambaye hakupenda kutajwa jina lake kwa madai yeye siyo msemaji alisema wateja hao hawakutendewa haki kwa sababu mmiliki wa deni hilo anafahamika ambaye ni Mbeya retco aliyemuuzia kanisa katoliki hivyo ilikuwa ni jukumu la kuwatafuta na kuwabana wahusika hao badala ya kuwaonea walala hoi hao.
 
Mfanyakazi mwingine alitoa ushauri kuwa wateja hao waonanne na uongozi wa kanisa ambao walinunua majengo hayo na kuwaomba waende katika shirika la Tanesco kwa kuandika barua kuwa hawakununua nyumba na madeni hili deni hilo liingie katika akaunti ya Mbeya Retco badala ya wapangaji hao.
 
Gazeti hili limepata nakala ya Ankara ya umeme iliyoandikwa" LUKU Sms operator fungua luku meter no.01319959639 ameshalipa deni lote bado kufuta riba chini kukiwa na sahihi yake julai,18,2011, na chini yake kukiandikwa ujumbe mwingine uliosainiwa na ofisa mwingine ukisema ," SRA mteja hana deni kiasi kilichobaki ni interest imeshaandikiwa bado kufutwa."
 
Hata hivyo gazeti hili lilikwenda kwa undani zaidi kuangalia jina la akaunti hiyo ambayo inatumika na wateja hao wanaodaiwa kubambikiwa ni Mr.Prince M John P.O.BOX 109,Mbeya ambayo ilonesha kuwa na deni la Sh.200,000 iliyopokelewa na kubakia Sh.1,566.05 katika nambari ya hesabu Prop Ref:T87.09.09203,cust Ref:85006773.
 
Wananchi hao walisema kuwa matumaini ya kuendelea kupata huduma ya umeme wa Tanesco yametoweka kabisa na kwamba wapo walala hoi kama wao waliobambikiwa madeni kama hayo na kwamba endapo Waziri wa nishati na madini atalivalia njuga suala hili kwa shirika la tanesco Mbeya na kwingineko watanzania watarudi katika dhama za mkolono kutumia vijinga vya moto na koroboi.
 
Meneja wa Shirika la Tanesco Mbeya,John Bandiye akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu aliulizia nambari ya akaunti ya mita na baada ya kupewa aliwaomba walalamikaji kufika ofisi ya Tanesco ke kwa ajili ya kueleweshwa kuhusiana na tatizo hilo ambapo baada ya kumjibu kuwa walishapewa kutoka kwa ofisa aliyekuwa akilishughulikia suala hilo hakuweza kujibu tena hadi tunakwenda mtamboni.
 
Mwisho.

No comments:

Post a Comment