Translate

Friday, December 7, 2012

JINAMIZI LA AJALI LAENDELEA KUUTESA MKOA WA MBEYA. Wawili wapoteza maisha, werngine kumi wajeruhiwa vibaya.




Moses Ng’wat na Thompson Mpanji, Mbeya.

WATU wawili , akiwemo mtoto  mdogo wamepoteza maisha na  wengine 10 kujeruhiwa vibaya katika ajali, mkoani Mbeya , baada ya Lori la mizigo kuzigonga na kuzitumbukiza Mtaroni Daladala mbili zilizokuwa zimeegeshwa kituoni.

Tukio hilo lilitokea jana majira ya saa 5:30 katika eneo la Kalobe baada ya Lori la Mizigo lenye namba za usajili T 7821 BVD  lililokuwa likielekea nchini Zambia kuzigonga gari mbili za abiria (Daladala) zenye namba za usajili T 945 AFJ na T 150 AJL  zilizokuwa zimeegeshwa katika kituo cha Njia Panda eneo la Kalobe Jijini hapa.

Kwa mujibu wa Muuguzi Mkuu wa Hospitali ya Ruufaa ya Mbeya, Thomas Isidory, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba walipokea maiti ya mtu mmoja ambaye hata hivyo jina lake halikuweza kupatikana licha ya kukutwa na tiketi yenye jina moja la Joshua, huku kifo cha mtoto huyo mdogo kilitokea wakati akipatiwa matibabu katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

Alisema kwa upande wa majeruhi waliopokelewa Hospitalini hapo,  walikuwa 10,  ambapo kati ya hao wawili hali zao zilikuwa mbaya na wamelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi wenye kuhitaji uangalizi maalumu (ICU).

Hata hivyo Isidory  alisema kati ya hao waliolazwa chumba cha wagonjwa mahututi ni mmoja tu aliyetambuliwa  kwa jina la Jane Mligo(19), ambaye ni mwanafunzi wa chuo cha ufundi VETA Mbeya, ambapo mwingine hakuweza kutambuliwa mara moja.

Aliwataja majeruhi wengine nane ambao wamelazwa katika Wodi za kawaida hospitalini hapo kuwa ni Jose Kalale (28) ambaye ni dereva wa moja ya Daladala hizo mbili zilizogongwa zikiwa kituoni, pamoja na Kondakta wake Elia Ambakisye.

Wengine ni Willy Claud (34), Winnie Ipyana(22), God Sanga (23), Josia Choga (28), Said Omary (18), pamoja na  mtoto mdogo, Nasra Japhary, ambaye hata hivyo umri wake haukuweza kupatikana mara moja .

Kwa upande wake mmoja wa majeruhi hao waliolazwa hospitalini hapo katika wodi namba moja, Josiah Choga, akisimulia tukio hilo, alisema yeye alikuwa akitokea katika Mji wa Mwanjelwa na walipofika eneo la Kalobe Daladala aliyopanda iliegesha kituoni wakati watu wakishuka na ghafla alisikia kishindo kikubwa kikitokea kwa nyuma .

“Pale kituoni kulikuwa na Daladala Mbili yakwetu ilikuwa mbele ghafla nilisikia kishindo kikubwa na nilipojaribu kugeuka nyuma nilishangaa Daladala tuliyokuwemo ikipigwa na kuanza kubingilika hadi mtaroni” alisimulia Chonga.

Aliongeza kuwa wakati akiwa wamefunikwa ndani ya Mtaro alishangaa kundi la watu wakifika na kuanza kuwachomoa toka ndani ya Daladala hilo huku akishuhudia baadhi ya abiri wakichuruzika damu nyingi mwilini mwao.

Naye Nsubiri Kibopile, ambaye ni mashuhuda wa ajali hiyo, alisema Roli hilo liliziparamia Daladala hizo baada ya kulikwepa gari lililokuwa likitokea mbele yake ambalo lilikuwa limebeba shehena ya vinywaji  vya moja ya kampuni ya vinywaji baridi.

“Huyu bwana wa Roli anaonekana tayari alikuwa ameharibikiwa na Breki hivyo akawa anashuka nalo na alipofika hapa kituoni aliojikuta akibanwa na lile fuso  lililobeba Soda  hivyo kuamua kutanua  na ndipo alipozivaa zile Daladala na kuzitumbukiza Mtaroni” Alisema Kibopile.

Hata hivyo baadhi ya askari wa kikosi cha usalama barabarani waliokuwepo katika eneo la tukio waliozungumza na Jambo Leo kwa masharti ya majina yao kutoandikwa gazetini kwa kuwa wao si wasemaji wa jeshi hilo, walidai ajali hiyo ilisababishwa na Roli hilo la mizigo baada ya kuharibika mfumo wa Breki.

“’Unajua hilo Roli lazima lilikuwa ‘limefeli’  ndio maana baada ya kuzigonga zile Daladala lilienda kusimamia mbali zaidi ya nusu kilomita, hata hivyo tunamshukuru mungu madhara hayakuwa makubwa kwani lingeweza kuacha njia na kwenda kuvamia  nyumba ” alisema mmoja wa askari hao.

Mwisho.


No comments:

Post a Comment