Translate

Monday, December 24, 2012

Baada ya ARVs sasa tiba asili yachakachuliwa

Na Thompson Mpanji,Mbeya
 
WAKATI Serikali na baadhi ya mashirilka na watu mbalimbali wakikesha na kukuna vichwa wakitafuta tiba ya maambukizi ya virusi vya ukimwi,hali imekuwa tofauti kwa baadhi ya watanzania wasio na mapenzi mema kwa watu wanaopata maradhi hayo baada ya kuanza kuchakachua dawa na vyakula vya asili zinazodaiwa kuwasadia kwa asilimia kubwa kuwapatia nafuu wagonjwa wenye maambukizi.
 
Itakumbukwa kuwa hivi karibuni serikali kupitia mamlaka husika iliingia mzozo na hata kufikia kuzuia baadhi ya dawa zinazotolewa na shirika moja nchini kutokana na madai ya kutengeneza dawa feki za ARVs jambo ambalo lilileta sintofahamu na hata wahusika kuamua kutolea ufafanuzi wa sakata hilo ambalo lilidaiwa kuingiliana na masuala ya kisiasa na maslahi binafasi ya watu.
 
Wataalamu wa tiba asili nao wameanza kupaza sauti zao kupitia vyombo vya habari kuiomba serikali na mamlaka husika kuingilia kati na kuwadhibiti maharamia hao wa tiba na vyakula asili ambazo zimekuwa zikiwasaidia watanzania walio wengi wenye maradhi sugu na maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa gharama nafuu na hatimaye kurudisha matumiani ya kuendelea kuishi na familia zao, sanjari na kufanyakazi.
 
Akizungumza na gazeti hili mmoja wa wajasiliamali wanaotengeneza `vyakula na tiba za asili kupitia matunda ya Ubuyu na Mlonge, Racher Alfan Mwasajone almaarufu Mama Peter,Mkazi wa Dodoma mtaa wa Makulu ya Njedengwa alisema wameingiliwa na maharamia wa madawa na kuanza kutengeneza bidhaa feki ambazo zimeanza kuonekana kutowasaidia tena na kuondoa matumaini kwa watu waliokumbwa na maradhi sugu ikiwemo Ukimwi.
 
Mjasiliamali huyo ambaye alihudhuria maonyesho ya wajasiliamali jijini Mbeya hivi karibuni alisema uchakachuaji huo unafanyika hasa katika mafuta ya ubuyu na mlonge na sasa wameingia katika unga wa ubuyu na mlonge kwa kuchanganya na unga mwingi wa mahindi ama muhogo ambapo kwa upande wa mlonge wanachanganya na majani ambayo hayaeleweki jambo ambalo linapunguza nguvu ya viini lishe vinavyokwenda kusaidia kinga ya mwili na kutibu maradhi mengine zaidi ya 40.
 
Racher alisema watu hao wasio na chembe ya huruma wamekuwa wakichanganya mafuta ya alizeti ama mafuta ya karanga katika mafuta ya mlonge na ubuyu na kuuza kwa bei ya chini huku wahitaji wakiyanunua kutokana na unafuu wa bei baada ya kupata ushuhuda ama historia ya kazi yake lakini matokeo yake hawapati aueni aidha kutokana na kutokana na ukosefu wa viini lishe katika bidhaa hizo feki ama vitu vinavyochanganywa kuwa sumu na kuuwa viini lishe.
 
Amefafanua kuwa ili kubaini mafuta ya ubuyu ama mlonge yaliyo safi ni vema kuangalia wepesi wa mafuta wakati wa kuinamisha chupa iliyokuwa na mafuta chini juu ambapo kwa unga wa ubuyu utajulikana kuwa ni halisi kwa kupata radha halisia ya ubuyu ambapo kwa majani ya mlonge hayana ukali na unga wake unanukia harufu nzuri ya kipekee inayomshawishi mtumiaji kunywa ama kulamba.
 
Hata hivyo Racher ametoa wito kwa serikali kupitia mamlaka husika kufuatilia kwa kina uhalifu huo na kuudhibiti kwani unaweza kuleta madhara makubwa kwa watumiaji wanaohitaji kupata tiba na hatimaye kuendelea kupoteza nguvukazi ya taifa kwa uzembe,makosa na tamaa ya watu wachache wasio na mapenzi mema na watanzania wenzao.
 
Mwisho.

No comments:

Post a Comment