Na Thompson Mpanji,Mbeya
TANZANIA ipo katika utekelezaji wa millennia ambayo ni matokeo ya
mkutano wa kilele wa millennia wa umoja wa mataifa uliofanyika mwezi
septemba mwaka 2000 na kutokana na hali hiyo sitegemei kuwa kuna
mtanzania asiyejuwa malengo hayo nane.
Lakini kwa kukumbushana ningependa kuyarejea tena maleongo hayo
yaliyopangwa kutekelezwa katika mataifa 189 ambayo yalikuwa ni
makubaliano yanayozitaka nchi zote zilizoendelea na zinazoendelea
kufanyakazi kwa pamoja na kuhakikisha umaskini na njaa duniani
vinatokomezwa,kuhakikisha elimu sawa kwa watoto wote,usawa wa jinsia na
uwezeshwaji kwa wanawake.
Malengo mengine ni kupunguza vifo vya watoto wachanga,kuokoa maisha
ya akina mama wazazi,kupunguza na kutokomeza ugonjwa wa ukimwi,marali
na magonjwa mengine maambukizi,kudumisha usafi na ubora wa mazingira
pamoja na kudumisha ushirikiano wa kimataifa kwa maendeleo kwa ujumla
malengo ya millennia yanasisitiza zaidi maeneo ya afya,elimu,mazingira
na ustawi wa jamii kwa ujumla.
Disemba,4,2012 kumefanyika tukio muhimu na la kihistoria kwa taifa
la Tanzania kutokana na kuwa miongoni mwa nchi 50 kati ya 189
zilizochaguliwa kujadili,malengo hayo nane ya millennia katika kanda
saba ambazo mahali yalipofanyika katikamabano ni kanda ya Ziwa
(Mwanza),kanda ya kaskazini (Arusha),Kanda ya kati(Dodoma),kanda ya
nyanda za juu (Mbeya),kanda ya kusini(Mtwara),kanda ya magharibi
(Shinyanga) na kanda ya mashariki (Morogoro).
Katika kutekeleza hili,John kajiba mtafiti kutoka taasisi ya
utafiti wa mambo ya uchumi na jamii (ESRF-Economic and Social Research
Foundation) anasema taasisi hiyo imeombwa kusimamia majadiliano hayo kwa
kushirikiana na Ofisi ya rais tume ya mipango katika kanda hizo saba na
hasa katika maeneo ya Serikali za mitaa,Asasi za kiraia,watoto,wazee na
wanawake wadogo ambapo kwa kanda ya Mbeya yamefanyika katika ukumbi wa
Hoteli ya Paradise,Soweto,jijini Mbeya.
Kajiba anasema kwa kuwa imebakia miaka mitatu ili kukamilisha miaka
15 iliyopangwa kufikia malengo ya millennia 2015 hivyo watu na taasisi
mbalimbali zimeona ni bora kuanza kujadili na kujiuliza kitatokea nini
na nini kifanyike baada ya mwaka 2015 ili kuongeza kasi na kutoa msukumo
wa maendeleo duniani.
Kwa mujibu wa taarifa ya ESRF kuna mafanikio na changamoto ambazo
zimejitokeza katika utekelezaji wa malebngo ya millennia ambapo kwa
upande wa Tanzania imefanya vizuri katika maeneo mengi,licha ya baadhi
ya maeneo kuwa na matokeo ambayo hayakuridhisha.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Abbas kandoro ambaye alikuwa mgeni rasmi
aliyefungua mkutano huo wa mashauriano katika hotuba yake amesema
utekelezaji wa Tanzania unategemea utekelezaji wa kila Mkoa na Wilaya na
hivyo ni dhahiri utatofautiana.
Ametolea mfano kwenye eneo la Ukimwi,Mkoa wa Mbeya una asilimia 9.2
kwa takwimu za mwaka 2008 wakati kitaifa ni asilimia 5.7,kupunguza
umaskini kitaifa imetokea asilimia 39 kwa mujibu wa takwimu za mwaka
1990 hadi asilimia 33.6 kwa takwimu za mwaka 2007.
Kandoro anasema pato la mkazi wa Mbeya ni juu ya dola 1 hadi 1.5
kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2010 ambapo katika elimu ya msingi na
Sekondari ukiangalia katika uwiano wa Ke na Me wamevuka lengo kama nchi
kwa asilimia 101 na 205 na kwa Mkoa wa Mbeya ni asilimia 102 na 88
ambayo kwa ujumla haijavuka lengo.
Anasema lazima kukiri kuwa bado kuna changamoto katika kutokomeza
umaskini wa kipato,njaa,kuboresha afya ya uzazi na huduma za maji salama
pamoja na elimu.
Kandoro ametoa maoni kuwa endapo kila mtanzania atajituma katika
kutafuta maisha na kuzitumia fursa zinazomzunguka,akaacha kuwa
mnung’unikaji wa hali ngumu ya maisha huku amekaa kijiweni,akaacha
kumtafuta mchawi kwa kila linalomsibu,akawa mchangiaji katika
kuhakikisha hali ya utulivu na amani inadumishwa kwa kuheshimu misingi
ya utawala bora,kasi ya kuliendeleza taifa itakuwa kubwa.
"Kwa sasa bado tunaongea sana, ‘we are talking a lot,’ninaamini
mkusanyiko huu utasaidia sana kufanya tathmini ya pamoja kujuwa
tulikotoka,tulipo na tunakokwenda,ninaipongeza serikali kuteuwa Taasisi
ya utafiti katika Nyanja za uchumi na jamii (ESRF) ifanye kazi ya
kukusanya maoni ya wadau mbalimbali,"anasema.
Mkuu wa Mkoa huyo amesema kupitia warsha kutoka katika mikoa yote
Tanzania, anao uhakika,ushauri na mapendekeo ya washiriki kuhusu kuamua
nini kifanyike kwa siku zijazo baada ya 2015 ni muhimu sana.
Kutokana na mpango wa millennia mataifa makubwa yaliyoendelea
yalipangiwa kutoa asilimia 7 ya pato lao la ndani kuchangia nchi
zinazoendelea ambapo ni asilimia 4 ya nchi za Scandinavia zimeonekana
kuongoza katika kuchangia ingawa siyo kwa asilimia zote na hiyo ni
mojawapo ya changamoto kubwa iliyozikumba nchi nyingi tegemezi kukwama
katika mipango na miradi yao ya maendeleo baada ya kukwama kwa misaada.
Dkt.John Mduma mwezeshaji ambaye ni Mhadhiri kutoka chuo kikuu cha
Dar es salaam anasema lengo la mashauriano hayo ni kutoa kichocheo cha
mjadala wa wadau mbalimbali,kujenga taswira ya kimataifa ya hali ya
baadaye kwa mapendekezo madhubuti,kuhakikisha na kusikika sauti za
maskini na wasio sikika,kutambua na kuchambua masuala yatakayoathiri
maendeleo,kushawishi mchakato ndani ya serikali kuu ioane na taasisi na
matokeo yanayotarajiwa.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment