Translate

Thursday, January 31, 2013

Mama adaiwa kumuuza mtoto ni baada ya kuwekeana mkataba wa kutunza mimba na 'wazungu',yadaiwa baada ya kujifunguwa Hospitali ya Ifisi Mbeya wazungu watoweka naye hakumuona hata sura,aliambiwa alimzaa mtoto wa kiume wa kilo 4,akienda kituo cha kulelea watoto Simike adaiwa kuoneshwa watoto yatima waliokotwa


Na Thompson Mpanji,Mbeya
MWANAMKE mmoja  Mkazi wa Mtaa wa  Ikuti,Kata ya Iyunga, jijini Mbeya  amedaiwa  kumuuza  mtoto aliyemzaa mwenyewe kwa wazungu  wanaomiliki kituo kimoja cha watoto yatima   cha jijini hapa ambao hadi sasa haieleweki walipo  pamoja na kichanga chake  kiume kinachodaiwa kuzaliwa  kikiwa na uzito wa kilogramu nne.
Tukio hilo ambalo limewasikitisha wananchi walio wengine  linadaiwa kutokea mwanzoni mwa Novemba,2012 ambapo makubaliano yanadaiwa kufanyika mwezi,oktoba,2012  katika maeneo  ya Ikuti  mbele ya mashahidi  likiwepo  kampuni  moja la  mwanasheria  wa kujitegemea  la jijini Mbeya.
Mwenyekiti wa mtaa wa Ikuti,Kata ya Iyunga,Immanuel Mwasote amekiri kuwepo kwa tukio hilo  na kumtaja mwanamke huyo kuwa ni Amina Nganile ambaye alikuwa akiishi katika mtaa huo na alikuwa mjazito  na  wenzake kuthibitisha alijifungua salama  lakini baada ya siku mbili alionekana bila mtoto jambo lililowashtusha wengi na kumfikisha ofisini kwake kwa kesi mbili.
Mwasote amesema  Amina alifikishwa ofisini kwake  na wanakikundi  wenzake wa kikundi cha Tumaini kwa madai ya kushindwa kurejesha deni la mkopo katika shirika la Eclof sanjari na kumhoji  alikompeleka mtoto  ambapo alijibu yupo ustawi wa jamii akiendelea kulelewa .
“Kutokana na majibu hayo tuliingiwa wasiwasi na ndipo tukampeleka katika kituo cha polisi Iyunga kwa mahojiano na baadaye walimwachilia,kwa hiyo  tuliwaachia polisi waendelee na uchunguzi na baadaye amehama mtaa wangu sijuwi alipokwenda,”amesema.
Akizungumza na Mwandishi wa  gazeti hili Msimamizi wa kikundi Tumaini ,Winfrida Nzunda  amesema  mwenzao huyo  alipokuwa mjamzito   walikuwa wakija wazungu na gari ambalo nambari zake hawakuzishika na kumchukuwa kumpeleka kuhudhuria  kliniki katika Hospitali ya Ifisi na kumrudisha hadi alipojifungua  na kulazwa  siku moja na kutoka bila mtoto.
Winfrida amesema  baada ya kumhoji  alielezea kuwa   baada ya kujifungua  hakuiona sura ya mtoto wake  baada ya kuchukuliwa na wazungu  hao ambao walikuwa wanawake wawili na wanaume watatu zaidi ya kumfahamisha kuwa  amejifungua mtoto wa kiume mwenye uzito wa kilo nne  na kwamba hadi leo haelewi  alipo mtoto wake  na wazungu hajawaona tena.
“Lakini baada ya kumbana sana alituambia kuwa Mama yake huyo aliyemtaja kwa jina la Mama Kasile  anayesimamia kituo cha kulelea watoto cha  For Care & Share-Children’s  Home kilichopo Simike jijini Mbeya  ndiye aliyemshawishi  kuwekeana mkataba na wazungu hao kumhudumia  hadi atakapojifunguwa  baada ya kutomjuwa mwanaume aliyempa mimba  na ndipo watamchukuwa mtoto kumlea hadi baada ya miaka 18  watamrejesha kwake,”amesema.
Msimamizi huyo wa kikundi amesema kuwa  baada ya kumbana zaidi aliwaeleza kuwa  mkataba wa kumhudumia ulimalizika  baada ya kujifungua na hivyo  wazungu hao  walimchukuwa mtoto huyo  na kwamba alipotoka Hospitali alikwenda kwa Mama Kasile ambako alihudumiwa kwa siku nne na baadaye kufukuzwa  kwa madai akajitegemee.
Amesema mwanamke huyo amethibitisha kuwa amedhurumiwa fedha na Mama  huyo kwani ana imani amepewa fedha nyingi  na kwamba katika hatua ya kushangaza  akifika kumwangalia mtoto anaoneshwa wale waliokotwa na kupewa muda wa dakika mbili  aondoke jambo ambalo linathibitisha kuwa mtoto wake ameshatoroshwa kwenda mashariki ya mbali.
Hata hivyo Winfrida amesema kuwa baada ya tukio hilo mwanamke huyo  amehama hapo mtaa wa Ikuti na haileweki anapoishi maeneo ya Nzovwe  na wanaendelea kumsaka  kutokana na kushindwa kurejesha deni la zaidi ya Sh.370,000 katika shirika la mikopo la Eclof  na hivyo wanahofia kufikishwa mahakamni kutokana na deni  la mwenzao huyo.
Meneja wa shirika la mikopo midogo  la Eclof tawi la Mbeya,Magdalena  Lekaaya amethibitisha kukopeshwa  Amina Nganile mkopo wa Sh.400,000 na kutakiwa kurejesha Sh.79,000 kila mwisho wa mwenzi pamoja na wanakikundi wenzake  lakini  baadaye hakuonekana hadi  wanakikundi walipomkamata.
Amesema baada ya kumhoji  na kumtania kwanini ameshindwa kurejesha mkopo ilhali ameshamuuza mtoto  alikiri na kudai hajapewa hata senti moja  na kwamba hana uwezo wa kulipa deni  wamfikishe kokote  na hivyo kumuona  kama amechanganyikiwa na kumwagiza aende kutafuta  hela hiyo chini ya udhamini wa wanakikundi wenzake lakini hajaonekana.
Baadhi ya ndugu,jamaa na marafiki wa Amina kutoka katika kijiji cha Isongole Umalila,wilaya ya Mbeya vijijini  wakizungumza  na gazeti hili wamesikitishwa na kulaani vikali tukio hilo na kjuiomba serikali  iweze kuchukuwa mkondo wake.
Gazeti hili linayo nakala ya mkataba wa makubaliano ya kumuuza mtoto huyo  baada ya ‘wazungu’ hao kutunza mimba  ya mwanamke huyo aliyetajwa kwa jina la Amina Paulo Nganile  na mtoto atayezaliwa  hadi afikie umri wa miaka 18.
Nakala ya mkataba huo una masharti sita yaliyoainishwa  katika kutimiza makubaliano  yaliyofanywa Oktoba,5,2012 kati ya kituo cha kulea watoto maarufu “Watunzaji’ Care & Share-Children’s home wa S.L.P. 573,Mbeya-Tanzania,East Afrika Phone No.0252502749 na Amina Paulo Nganile anayeishi karibu na Itende JKT,eneo la Nzovwe,Mbeya ambaye kwa upande mwingine anaitwa MAMA MZAZI.
Sehemu ya makubaliano hayo yameandikwa kama ifuatavyo:” kwamba watunzaji ni wenye kumiliki kituo cha kulelea watoto wadogo chini ya umri wa miaka 18,kwamba kwa hiari yao watunzaji  na kwa hiari ya MAMA MZAZI ambaye ni mjamzito wamekubaliana  kuwa MAMA MZAZI atatunzwa  na kituo hicho yeye mwenyewe na kusaidia gharama za kujifungua mtoto.
“Kwamba baada ya mtoto kuzaliwa ‘watunzaji’ wataendelea kumtunza  mtoto atakayezaliwa mpaka atakapofikia umri wa miaka 18,kwamba baada ya mtoto kufikisha umri wa miaka 18 ‘mama mzazi ‘ataruhusiwa kumchukuwa mtoto  wake,kwamba matunzo kwa mama mzazi yatakoma mara baada ya kujifungua.”
Sharti la sita limesema,” kwamba MAMA MZAZI hamjuwi aliyempa mimba na hivyo hana uwezo wa kutunza mimba na mtoto atayezaliwa  hivyo anakubali kuwa mtoto atayezaliwa atunzwe  na ‘watunzaji ‘hadi atakapofikia umri wa miaka 18.”
Aidha sehemu ya mkataba huo imesema makubaliano hayo yametiwa sahihi na wahusika wote  mbele ya mwanasheria ambaye ni  Melvin Kauffman wa For care & share-children’s home na ‘Mama Mzazi’ Amina Paulo Nganile na shahidi aliyeandikwa kwa jina la Anna Kasile mwenye nambari ya simu 0754 615021 mbele ya Wakili kutoka kampuni ya Mwakolo and Co.Advocates,P.O.BOX 2908,Mbeya-0754052231 ikiwa imewekwa na mhuri wa kampuni hiyo ya mwanasheria wa kujitegemea.
Jitihada za kumtafuta ‘mama mzazi’ ambaye ni mama wa  kichanga cha kiume   kilichozaliwa na uzito wa kilo nne  zinaendelea ili kupata ukweli  wa tukio hili ambapo anayedaiwa mama mkubwa aliyemshawishi  kumuuza mtoto huyo  alipopigiwa simu  na kuhojiwa kuhusiana na tukio hilo alijibu kwa jazba kuwa hasipotezewe muda
Anna Kasile ambaye anadaiwa kuwa ni mama mkubwa,msimamizi wa kituo aliyekuwa  muda wote na 'wazungu' hao alimwambia mwandishi wa habari hizi kuwa  amuulize vizuri Amina sababu ya yote hayo na ikiwezekana amtafute aende naye kituoni hapo.
Kasile amesema  amehojiwa na watu wengi  ikiwemo waandishi wa habari na polisi kwa hiyo amechoka kujieleza, hawezi kupoteza muda kwa ajili ya masuala ya kipuuzia na hatimaye alikata simu na alipopigiwa zaidi ya mara nne alikata simu licha ya kutumiwa ujumbe mfupi wa maandishi kufafanua tuhuma dhidi yake kuwa amekuwa na kawaida ya kuwauza watoto anaowaokota wametupwa na kuwalea hakujibu.
Jitihada  za  kuwasiliana na Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya,Diwani Athumani,a Kampuni ya Wakili Mwakolo(Mwakolo and Co. Advocates)  na Ofisi ya ustawi wa jamii  Mkoa wa Mbeya kujuwa  utaratibu wa kuasili watoto na mkataba wa makubaliano  zinaendelea.
 Mwisho.

No comments:

Post a Comment