Translate

Sunday, September 8, 2013

Chadema walonga maisha ya wanachunya



LICHA ya kuwa na utajiri mkubwa wa madini ya Dhahabu katika Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya, bado wananchi na wakazi wa wilaya hiyo wanaendelea kuteseka kwa ukosefu wa maji safi na salama.

Tatizo la maji limeshindwa kupatiwa ufumbuzi  katika Wilaya hiyo kwa muda mrefu sasa ambapo wadau mbali mbali wameshauri Serikali kufanya kama ilivyofanya Mkoani Shinyanga kuchukua maji Ziwa Victoria kilomita zaidi ya 700.

Wamesema Wilaya ya Chunya ina Ziwa Rukwa ambalo lingeweza kusaidia kujenga mradi wa maji na kuwaondolea adha wananchi wa Chunya ziwa ambalo liko umbali usiozidi kilomita 50 hivyo kupunguza gharama kama zilizotokea Mkoani Shinyanga.

Ushauri huo ulitolewa jana na Katibu Mwenezi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Lukasi Mwampiki, alipokuwa akihutubia wananchi wa Kijiji cha Saza Wilayani Chunya katika ziara ya kuimarishja chama inayoendelea Wilayani humo.

Alisema katika kijiji cha Saza ambacho kwa miaka hamsini tangu uhuru hawajawahi  kupata huduma za maji safi na salama licha ya kuwepo kwa mgodi mkubwa wa madini ya dhahabu inayochimbwa na wawekezaji wa nje.

Alisema kukosekana kwa Maji katika Wilaya hiyo ni aibu kubwa na inaonesha dhahiri Mwekezaji kutowajali wananchi ambapo pia hawanufaiki na uchimbaji huo ambao umeshindwa kuwatatulia tatizo sugu la maji linalowakabili wananchi hao kwa muda mrefu.

Mwampiki alisema Serikali inaweza ikatumia njia rahisi kama ilivyofanyika Mkoani Shinyanga ambako tatizo la maji limetatutiliwa kwa kuchukuliwa maji katika Ziwa Viktoria lililo umbali wa zaidi ya Kilomita 700 ili hali ziwa Rukwa likiwa jirani kabisa na Wakazi wa Chunya ambao wanaweza kusahau kabisa shida ya maji.

Alisema maji ya Ziwa Rukwa yakichukuliwa  yataondoa gharama na adha wanayoipata Wananchi kwa kusafiri umbali mrefu kutafuta maji huku wakishindwa kufanya shughuli zingine za maendeleo hususani wanafunzi ambao hushindwa kuhudhuria masomo ambapo bado maji yanayopatikana kutofaa kwa matumizi ya binadamu.

Aliongeza kuwa wananchi walitakiwa kushirikishwa kabla ya mwekezaji hajaanza uchimbaji wa madini ili apewe vipaumbele vitakavyo wanufaisha moja kwa moja likiwemo tatizo sugu la maji ambalo alitakiwa alitatue kabla ya kazi yoyote.

Aidha katika hatua nyingine Mwampiki aliwashauri wananchi wa Kijiji cha Saza kuwahoji Madiwani wao kuhusu hati chafu zinazotolewa na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali(CAG) kwa Halmashauri na wao kuziangali tu na kukosesha sifa Halmashauri kwa matumizi mabaya ya fedha za wananchi.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment