Na Thompson Mpanji,Njombe
BENKI ya wananchi wa Mkoa wa Njombe(NJOCOBA) imefanikiwa
kutoa mikopo ya zaidi ya Sh.Bil.3.6 hadi
kufikia disemba ,mwaka 2011 kwa wananchama wake ikiwa ni mkakati wa kuboresha hali za maisha ya wananchi wa Mkoa
wa Mbeya.
Aidha Njocoba imefanikiwa kuingiza mapato ya Sh.Mil.554
ambapo faida kwa mwaka ilifikia
Sh.Mil.10 ingawa imeelezwa kuwa benki hiyo ilipata hasara ya Sh.Mil.289 iliyotokana na gharama kubwa za
uanzishwaji wa benki ambazo Benki kuu (BOT) iliamuru kuhesabika kama matumizi
ya awali kabla ya benki kufunguliwa.
Akitoa taarifa fupi tangu kuanzishwa kwa benki hiyo mbele ya Mkuu
wa Mkoa wa Njombe,Kapt.mstaafu Aseri Msangi,Mwenyekiti wa Bodi ya Benki hiyo,Bi. Twilumba
Ulaya amesema tangu kufunguliwa rasmi
kwa benki hiyo septemba,13,2010 ilianza na zaidi ya sh.Mil.15.8 imekuwa na
maendeleo mazuri kwa wananchi kuhamasika kujiunga hadi
kufikia wateja 5,099 kwa kufungua akaunti mbalimbali.
Amesema benki hiyo
hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2011 imefikisha amana ya zaidi ya Sh.Bil.1.8
katika akaunti za akiba,biashara,muda
maalum katika akaunti za makundi maalum,binafsi,makampuni,taasisi,watoto na
wanafunzi na ushirika.
Mwenyekiti huyo amesema katika kipindi cha mwaka 2011 zaidi
ya hisa 55,000 zenye thamani ya Sh.Mil.55 zilinunuliwa na hivyo hisa za benki zilifikia 442,000
zenye thamani ya sh.Mil.442 ambapo mtaji uliopo hadi kufikia juni ,2012
umefikia zaidi ya Sh.Mil.290 kiasi ambacho ni chini ya mtaji unaotakiwa na ununuzi wa hisa wa Sh.Mil.500
na hivyo kuwaomba wanachama kuongeza ununuzi wa hisa.
Bi.Twilumba amesema urejeshaji wa mikopo siyo mzuri kwani kwa kipindi hicho mikopo ambayo ni
mibaya na hailipiki vizuri ni zaidi ya
Sh.Mil.267 sawa na asilimia 18 ya mikopo yote na kwamba tayari kesi tatu za madai zenye thamani ya zaidi ya Sh.Mil.72.4 hadi
kufikia juni,30,2012 zimeshafunguliwa katika mahakama ya wilaya ya Njombe.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa
Njombe,Kapt.Msangi ametoa wito kwa wakazi wa Njombe kujiunga kwa wingi
katika benki yao na kwamba yeye atakuwa
mwanahisa na ataendelea kuhamasisha
wakazi wa Njombe wanaoishi Dar es salam na mikoa mingine ikiwemo na halamshauri
zote za Wilaya ya njombe kujiunga na benki hiyo.
Hata hivyo Kapt.Msangi ameuomba uongozi wa Benki ya Njocoba
na Bodi yake kuweka mikakati na taadhari kwa baadhi ya wanahisa wasije wakahodhi benki kwa
kununua hisa zote na hivyo wanachama kujikuta hawana chao na kumilikiwa na mtu
mmoja hali ambayo itaondoa dhana nzima ya neno Benki ya wananchi.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment