Translate

Sunday, August 25, 2013

Tamasha la TGNP lilete matumaini kwa wanawake


Na Thompson Mpanji,Mbeya

MTANDAO   wa jinsia Tanzania(TGNP) kwa kushirikiana na wanaharakati na wadau mbalimbali wanatarajia kushiriki Tamasha  mapema septemba,3,2013 ambapo litatoa nafasi  na fursa  kwa wanaharakati  zaidi ya 5,000 kushiriki kutoka ndani na nje  ya Tanzania.

Tukio hili la siku nne,linajumuisha uchambuzi,utafiti,uanaharakati,kujenga uwezo,sanaa vyote vikiwa  na matokeo dhahiri ili kutoa ama kuonesha ushuhuda wa yale yanayojiri miongoni mwetu.

Malengo ya tamasha la jinsia 2013 ni kusherehekea  miaka ishirini  ya harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi inayochangia upatikanaji wa haki za wanawake,usawa wa kijinsia na haki za kijamii.

Kuongeza  uelewa  wa  muktadha uliopo kimataifa,wa mfumo dume na uliberali mamboleo,madhara yake kwa wanawake walioko pembezoni na jamii zao,mapambano yao dhidi  ya mifumo chanya na mingine kandamizi,na mikakati mbadala kwa ajili ya ukuaji na maendelo endelevu yenye usawa na haki.

Aidha kuendeleza uelewa wa nadharia na vitendo  kwenye ukombozi wa wanawake kimapinduzi,ikiwa ni pamoja  na kutunza  kumbukumbu  za mapambano halisi dhidi ya mfumo dume na uliberali mamboleo,na jinsi ya kuimarisha  ukombozi wa wanawake kimapinduzi katika ngazi zote.

Tunasema hongera TGNP,wadau na wanaharakati wengine kuazimisha Tamasha hilo ambalo ninaamini litawapatia mwelekeo wenu katika harakati hizi za kumkomboa binadamu na hasa mwanamke.

Ninaweza kusema kuwa Tamasha hilo litasaidia kufanya ufuatiliaji na tathmini  kuhusu mlikotoka,mlipo na mnapoelekea katika harakati hizi ngumu ambazo kwa wakati mwingine zinahatarisha maisha na hivyo kuhitaji moyo wa kujitolea na kujituma zaidi kutoka ndani ya sakafu ya moyo,ndani ya mishipa na damu kwa ujumla.

Tunaamni kuwa tamasha hilo pia litawaweka pamoja na kupanga mikakati na mipango kazi  itakayotekelezeka katika ngazi zote kwa ajili ya ujenzi wa harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi nchini Tanzania,Afrika na dunia kwa ujumla.

Tamasha hili litasaidia kuimarisha  utambuzi,mitandao,ujenzi wa nguvu za pamoja na miungano ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi kama misingi  ya kuelekea tapo la ukombozi wa wanawake kimapinduzi wa Afrika.

Tunaambiwa kuwa katika Tamasha hilo kutakuwa na  Mada mbalimbali kama vile jinsia Demokrasia na maendeleo,miaka 20 ya harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi,haki na usawa wa kijinsia,tuko wapi na tunakwenda wapi,Mapambano  ya haki  ya ardhi na uchumi,rudisha rasilimali kwa wananchi,mapambano ya ukombozi wa  wanawake kimapinduzi kwa ajili ya Demokrasia kwenye vyombo vya kiserikali na visivyo vya kiserikali.

Mada nyingine ni pamoja na mabadiliko ya katiba au mapinduzi,Mapambano  ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi na ujenzi wa tapo miaka ishirini ijayo sanjari na ujenzi wa umoja wa Afrika kwa mtazamo wa ukombozi  wa wanawake kimapinduzi.


Kabla ya kuendelea tuangalie hili Shirika la TGNP linatoka wapi na linafanya nini katika jamii,ni miongoni mwa mashirika  yasiyo ya kiserikali yanayofanya jitihada mbalimbali katika kuhakikisha tatizo hili linakomeshwa kabisa  na kutoweka katika jamii ya kitanzania na dunia kwa ujumla.

Ni shirika  la kiraia na kiuharakati,linalotetea mabadiliko ya kijamii kwa mtazamo wa kifeministi ambayo yanalenga  kwenye usawa wa jinsia,ukombozi wa wanawake,haki za kijamii,kufikia na kumiliki rasilimali kwa wanawake,vijana  na makundi mengine  yaliyoko pembezoni.

Dhana ya TGNP ni kujenga tapo la mabadiliko  katika jamii,ambalo litachangia kuwepo kwa jamii yenye mabadiliko ambayo inatambua  na kuthamini masuala ya jinsia,demokrasia,haki za binadamu na haki za kijamii.

Kwa mujibu wa Ofisa uhusiano wa TGNP Kenny Ngomuo anasema septemba,3,2013 ni Tamasha  la jinsia  ambalo huandaliwa  na mtandao wa jinsia Tanzania(TGNP) wakishirikiana  na mtandao wa mashirika  watetezi wa haki za binadamu na usawa wa jinsia (FemAct),pamoja na washirika  wao wengine  kama mitandao ya jinsia  ngazi ya kati ( IGNs),zilizopo  katika ngazi za wilaya,makundi mbalimbali ya kijamii ambayo ni sehemu ya semina  za jinsia na maendeleo (GDSS) za TGNP, na vikundi vingine  ambavyo  vimetambuliwa  katika utafiti kuhusu harakati za ukombozi wa wanawake kimapinduzi (TFMB).

Ngomuo ansaema Tamasha la jinsia  ni nafasi ya wazi kwa ajili ya watu binafsi,mashirika na mitandao,walio katika mapambano yanayofanana,kubadilishana uzoefu,taarifa,kujengeana uwezo,kusherehekea mafanikio  na kutathmini changamoto zilizo mbele yao,kujenga  na kuimarisha mitandao,na kupanga kwa pamoja  mikakati kwa ajili ya kuleta mabadiliki  ya kijamii kwa mtazamo wa kifeministi,kujengeana uwezo ili kuchangia katika mijadala ya wazi kuhusu maendeleo ya jamii na binafsi.

Ofisa huyo anasema Lengo  kuu la tamasha  ni kuwaleta pamoja wanawake/wanaharakati wa kifeministi na wengineo,ambao wanawamini kwenye usawa wa jinsia na  ukombozi wa wanawake ,kutoka Nyanja zote za maisha ,kutoka vijiji na wilaya za Tanzania,na sehemu  mbalimbali duniani,kwa lengo la uanaharakati na ushirikishanaji wa taarifa  kwa masuala mahsusi.

Anasema taswira ya TGNP inafanya jitihada za kuwezesha ukuaji wa vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi lenye misingi yake katika jamii hivyo kupelekea kufanyakazi moja kwa moja na wanaharakati katika makundi ya kijamii,wanamtandao na makundi ya muungano  katika ngazi mbalimbali.

Ngomuo anasema mkazo mkubwa unawekwa  katika kukuza uwezo wa hayo makundi na mitandao ili yaweze kufanya uchambuzi wa kijinsia  na ujenzi wa nguvu ya pamoja katika kutekeleza mipango yenye kuleta mabadiliko ndani  ya jamii zao na kujenga  mahusiano na wengine  katika ngazi ya jamii ya taifa,kikanda na kimataifa.

Anafafanua zaidi kuwa dhima ya TGNP ni kuwa chachu katika ujenzi  wa harakati za vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi unaolenga kubomoa mfumo dume na mifumo mingine kandamizi ikiwepo ukoloni mamboleo,ubeberu na ubepari ngazi zote,kutetea,kushawishi na kushinikiza  uwepo wa usawa wa jinsia,ukombozi wa mwanamke kimapinduzi,haki ya kijamii.


Aidha Ngomuo anabainisha Dira yao ni kuwepo kwa jamii ya Tanzania inayoheshimu  usawa wa jinsia  na haki ya kijamii,kusimamia haki za jamii.

Hata hivyo anahitimisha kwa kuelezea mafanikio  kwa miaka 20 tangu TGNP ianzishwe ni kuwa imefanikiwa kushawishi sera za umma kuingiza masuala ya harakati za vuguvugu la ukombozi wa mwanamke kimapinduzi,ikiwepo kuingiza masuala ya usawa wa kijinsia na haki za kijamii kwenye mifumo na taasisi ikiwemo na kukuza hamasa na uelewa wa wanachama,washiriki na serikali,kila lakheri TGNP na wadau wengine katika Tamasha hilo ambalo litaongeza kasi,ari na nguvu ya kufanyakazi zaidi!!.

tmpanji@yahoo.com
www.mpanjimwanamai.blogspot.com
0765 813180

No comments:

Post a Comment